JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

HOTUBA YA KAMISHNA WA MAADILI BARAZA LA WAFANYAKAZI MACHI 2025
13 Mar, 2025 Pakua

HOTUBA YA KAMISHNA WA MAADILI, JAJI (Stahiki) SIVANGILWA S. MWANGESI KATIKA UFUNGUZI WA MKUTANO WA BARAZA LA WAFANYAKAZI WA SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA TAREHE12/03/2025 – UKUMBI WA MIKUTANO JENGO LA MAADILI- DODOMA

 

NDUGU,

MAKATIBU,

WAKUU WA IDARA NA VITENGO,

MAKATIBU WASAIDIZI,

VIONGOZI WA TUGHE,

WAJUMBE WA BARAZA LA WAFANYAKAZI,

WAGENI WAALIKWA,

MABIBI NA MABWANA.

 

Nawasalimu kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania!

 

Awali ya yote, ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kuwepo leo hii tukiwa na Afya njema.

Niwashukuru Watumishi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kutimiza wajibu wenu ipasavyo kwa uadilifu na weledi.

Natoa pongezi kwa waandaaji wa Mkutano huu, kwa maandalizi mazuri na kufanikisha kufanyika kwake.

Ninatambua huu ni mkutano wa pili wa Baraza la Wafanyakazi kwa mwaka wa fedha 2024/2025. Nawakaribisha wote katika Jengo letu ambapo ni Ofisi za Makao Makuu na Kanda ya Kati kwa wale ambao wanafika kwa mara ya kwanza.

 

Ndugu Wajumbe;

Mabaraza ya Wafanyakazi yameundwa kisheria kwa madhumuni ya kuishauri Serikali katika ngazi ya Taasisi ili kusimamia rasilimali na utekelezaji wa majukumu ya kila Taasisi ya Umma. Ninawaomba wajumbe wote mtumie fursa hii ya kuwawakilisha wenzenu vizuri ili Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma iweze kufikia malengo iliyojiwekea katika utekelezaji wa majukumu yake na kukidhi matarajio ya wananchi kwa ujumla.

Kukusanyika kwenu hapa iwe ni sehemu muhimu katika kuboresha mazingira ya kazi na pia kuongeza ufanisi na tija katika Taasisi yetu. Uzoefu umeonesha kuwa Mabaraza ya Wafanyakazi yanapotumika vyema, hali ya maelewano na utulivu mahali pa kazi huongezeka na hivyo kuongezeka kwa tija.

 

Ndugu Wajumbe;

Katika mkutano huu tutapata nafasi ya kupata uelewa kuhusu utekelezaji wa Bajeti ya mwaka 2024/2025 na Mwelekeo wa bajeti ya mwaka 2025/2026. Pia tutapokea taarifa ya Mfuko wa Kusaidiana na tutapatiwa elimu kuhusu mfuko wa amana wa UTT AMIS. Nawasihi kutumia vizuri muda huu kwa ajili ya kuchangia mawazo ambayo yataongeza tija kwa Taasisi yetu

Ndugu Wajumbe;

Pamoja na kuwa tumekutana maalumu kwa ajili ya kupokea na  kujadili utekelezaji wa bajeti ya Taasisi 2024/2025 na mwelekeo wa Bajeti 2025/2026 lakini ni fursa pia ya kukumbushana machache kuhusu namna bora ya utekelezaji wa majukumu yetu kwa mtumishi mmoja mmoja na Taasisi kwa ujumla.

 

Ninafahamu kuna baadhi yetu wana changamoto za kiuadilifu katika utendaji wao, lakini kwakuwa Taasisi yetu tunayoitumikia ni ya kimaadili basi hatuna budi kukumbushana kwa lengo la kujipa muda kujitathmini na kujirekebisha kwenye suala la uaminifu, nidhamu, kupendana pamoja na utii kwa mamlaka na viongozi waliopo juu yetu kwa kuwa hayo yote yana athari chanya katika utekelezaji wa majukumu yetu na taswira ya Taasisi yetu kwa ujumla.

Aidha, nasisitiza kwenu wajumbe mkawe mabalozi kwa watumishi wengine kwenye suala la ujazaji wa majukumu katika mfumo wa e-utendaji ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali na pia Waraka wa Ndani Na. 1 wa Mwaka 2025 ambao umetenga siku maaalum   ya Alhamisi ya kila wiki kwa ajili ya kuingiza taarifa za utendaji kazi katika mfumo.

 

Ifahamike kuwa jukumu kubwa la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ni kusimamia Maadili ya Viongozi wa Umma, hivyo ni muhimu kwa watumishi wa Taasisi yetu kuwa mfano wa kuigwa katika uzingatiaji wa maadili. Hii ni katika kutekeleza Kanuni ya pili ya Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma za mwaka 2023 “UTII KWA SERIKALI” ambapo mtumishi anapaswa kuzingatia na kutekeleza Sera, Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo inayoongoza utendaji kazi ikiwa ni kupokea na kutekeleza maagizo halali yanayotolewa na Viongozi wa Serikali.

Ndugu Wajumbe,

Kwa kuwa tumekubali kuwa watumishi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, niwakumbushe kwa mara nyingine kuwa tunawajibika kuzingatia nidhamu, uaminifu, uwazi na kupendana; atakayeenda tofauti na hayo atakuwa si miongoni mwetu na hatutasita kuchukua hatua stahiki.

 

Pamoja na changamoto nyingi tunazokabiliana nazo katika kazi yetu ya kusimamia uadilifu, ninawaomba tusikubali kuyumba au kuyumbishwa na hatimaye kutolewa kwenye mstari, tuendelee kufuata misingi ya weledi na maadili katika utendaji kazi kwa kuepukana na rushwa na kushinda vishawishi vya rushwa na tamaa nyinginezo.

 

Ndugu Wajumbe;

Binafsi nawapongeza kwa ushirikiano ambao mmenionesha. Ninaomba ushirikiano huo uendelee. Kwa upande wangu mlango uko wazi pale kwenye changamoto yoyote msisite kuniona ili tuijadili kwa pamoja na kuipatia ufumbuzi kwa ajili ya maendeleo ya Sekretarieti katika mchango wake wa KUDUMISHA UTAWALA BORA.

Aidha, kama mnavyonipa ushirikiano naomba ushirikiano huo uwe miongoni mwenu pia ili Taasisi ifike mbali.

 

Ndugu wajumbe,

Mwisho ninawashukuru kwa kuhudhuria na kila mmoja aendelee kufanya kazi kwa uadilifu, ubunifu na uzalendo wa hali ya juu kuhakikisha kuwa Taasisi yetu inafikia malengo yake. Ninawatakia majadiliano mema na yenye kujenga.

Baada ya kusema hayo, sasa natamka rasmi kuwa Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, UMEFUNGULIWA RASMI.

 

AHSANTENI KWA KUNISIKILIZA

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >