JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

PO-ETHICS SECRETARIAT Logo
KIONGOZI MMOJA AFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI
14 Jan, 2026
KIONGOZI MMOJA AFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI

Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma imemfikisha mbele ya Baraza la Maadili Mkuu wa Idara ya Mipango wa Halmashauri ya wilaya Mbogwe mkoani Geita kwa kukiuka Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Bw. Alex Manyama Mang’ara aliyekabiliwa na mashtaka manne tofauti alifikishwa mbele ya Baraza la Maadili tarehe 14 Januari 2026 katika ukumbi wa ofisi za Sekretarieti ya Maadili jijini Dodoma kujibu tuhuma zinazomkabili.

Wakili Mkuu wa Serikali Bw. Hassan Mayunga ameliambia Baraza kuwa Bw. Alex Manyama bila sababu za msingi ameshindwa kutimiza matakwa ya kifungu cha 6(1)(a) na 6(1)(c) vya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma hivyo, kukiuka maadili ya uongozi wa umma kwa mujibu wa kifungu cha 6(2) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

“Wakati akikaimu nafasi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbongwe  na akitekeleza majukumu yake alimuhamisha kituo cha kazi mtumishi wa Halmashauri hiyo Bi. Asifiwe Chipata na kumshusha cheo bila kuzingatia sheria, kanuni na taratibu.”

Wakili Mayunga aliongeza kuwa, “Kitendo hicho ni kinyume na kifungu cha 6(1) (c) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kinachosomeka pamoja na kanuni ya 3(2)(a) ya kanuni za udhibiti wa Mgongano wa Maslahi.”

Aidha, Wakili Mayunga alilieleza Baraza la Maadili kuwa, Mlalamikiwa pia alimhamisha kituo cha kazi mtumishi mwingine wa Halmashauri hiyo Bi. Mercy Kabaka na kumshusha cheo bila kuzingatia sheria, kanuni na taratibu kinyume na kifungu cha 6(1)(c) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi  wa Umma kinachosomeka pamoja na Kanuni ya 3(2)(a) ya Kanuni za Udhibiti wa Mgongano wa Maslahi.

Shtaka jingine linalomkabili Bw. Alex Mangara ni kumpanisha cheo Bw. Mohamed Manawa mtumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya  Mbogwe kuziba nafasi iliyoachwa wazi na Bi. Mercy Kabaka aliyemhamisha na kumshusha cheo.

“Mhe. Mwenyekiti wa Baraza la Maadili, kitendo hicho ni kinyume na kifungu cha 6(1)(c) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kikisomeka pamoja na Kanuni ya 3(2)(b) ya Kanuni za Udhibiti wa Mgongano wa Maslahi,” alisema.

Kosa la nne pia linalomkabili Bwa. Alex ni kummpandisha cheo Bw. Edmund Kowi mtumishi wa Halmashauri ya Mbogwe kuziba nafasi ilioachwa wazi na  Bi. Asifiwe Chipata  aliyemuhamisha na kumshusha cheo.

Kwa mujibu wa maelezo ya shtaka hilo, kitendo hicho ni kinyume cha kifungu cha 6(1)(c) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kikisomeka pamoja na Kanuni ya 3(2)(b) ya Kanuni za Udhibiti wa Mgongano wa Maslahi.

Baada ya kusomewa mashtaka, Mhe. Rose Teemba, Mwenyekiti wa Baraza la Maadili alimuuliza mlalamikiwa kama amesikia mashtaka dhidi yake na kama anakiri kutenda kosa, Mlalamikiwa alisema, “ni kweli nimesikia mashtaka dhidi yangu na ninakiri kutenda hayo makosa.”

Bw. Alex alisema, “kwa kuwa maelezo yote yaliyosemwa na vifungu vya sheria vilivyotamkwa sina neno zaidi ya kuomba kusamehewa. Nilifanya hivyo kwa kukosa umakini.”

Aidha, Mhe. Teemba alisema, kwa kuwa maelezo yametolewa na umekiri kwa kinywa chako, Baraza litafanyia kazi shauri hili. Unaweza kwenda.”

Baraza la Maadili linaongozwa na Mhe. Jaji (Mst.) Rose Teemba, akisaidiana na Wajumbe wa Baraza hilo Bi. Suzan Mlawi na Bw. John Samwel Mgetta.

Upande wa mashtaka uliwakilishwa na Wakili Mkuu wa Serikali Bi. Emma Gelani, Bw. Hassan Mayunga, Lydia Mwakibete na Catherine Tibasana.

    

 

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >