JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Waziri Simbachawene azindua Makubaliano ya ushirikiano kati ya Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Chuo cha Uhasibu Arusha.
06 Mar, 2025
Waziri Simbachawene azindua Makubaliano ya ushirikiano kati ya Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Chuo cha Uhasibu Arusha.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene (Mb) amezindua Mkataba wa Makubaliano ya ushirikiano katika nyanja mbalimbali kati ya Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma  na Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA).

Uzinduzi huo umefanyia tarehe 6 Machi, 2025 katika ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Simbachawene alisema kuwa makubaliano hayo yanaenda kuleta mwamko mpya kwa watu mbalimbali wa kuelewa suala la maadili na utawala bora kabla ya kushika nyadhida za uongozi wa umma.

“Nimeelezwa kuwa mmeingia makubaliano ya kutoa mafunzo kwa viongozi na watumishi wa umma katika nyanja mbalimbali, nitoe rai kuwa katika mafunzo yenu hakikisheni mnawaelimisha viongozi na watumishi matumizi sahihi ya mifumo iliyowekwa na Serikali kudhibiti mawasiliano ya ana kwa ana kati ya mtoa huduma na mpokea huduma. Uwepo wa mawasiliano ya ana kwa ana unachochea ukiukwaji wa maadili kwa kutoa ama kupokea rushwa na kusababisha kunyimwa haki kwa wanaostahili na kupatiwa wasiostahili,” alisema.

Aidha, Mhe Simbachawene alitoa raikwa  IAA na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kutoa mafunzo ya matumizi sahihi ya rasilimali za nchi ili kupata mafanikio chanya katika Taifa.

“Sote ni mashahidi tunaona jinsi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan anavyopambana kuhakikisha kwamba nchi inakua na rasilimali za kutosha, lakini juhudi zake zinarudishwa nyuma na baadhi ya viongozi na watumishi wasiokua waadilifu wanaotumia rasilimali za nchi vibaya. Niwaombe mkawafundishe watumishi namna nzuri ya ugawaji na utumiaji wa rasilimali hizi kwa manufaa ya wote.”

Katika hatua nyingine, Mhe. Simbachawene alisema kuwa viongozi wote na watumishi wa umma wanapaswa kuwa mfano bora wa uwajibikaji, uwazi na  utendaji haki kwani Taifa likiwa na Viongozi watenda haki tutajenga mfumo imara wa kuwahudumia wananchi kwa haki ili kujenga imani ya wananchi kwa serikali yao.

Katika maelezo yake ya utangulizi, Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi alieleza kuwa Mkataba wa Makubaliano kati ya Sekretarieti ya Maadili na Chuo cha Uhasibu Arusha, unalenga kuimarisha ushirikiano katika nyanja za utafiti wa maadili na utawala bora, utoaji wa ushauri wa kitaalam, machapisho kuhusu maadili na uongozi, pamoja na ujenzi wa mifumo madhubuti ya utawala bora.

Kwa mujibu wa Mhe. Mwangesi, mafunzo yatakayotolewa  baada ya makubalianao hayo  yatasaidia kuwaelimisha viongozi wa umma kuhusu umuhimu wa kuepuka mianya ya rushwa na matumizi mabaya ya madaraka.

 

“Maarifa watakayopatiwa viongozi na watumishi wa umma, yatawasaidia kupata uwezo wa kutambua na kushughulikia changamoto za kimaadili zinazoathiri utendaji wao na jamii kwa ujumla,” alisema.

 

Katika hatua nyingine Mhe. Kamishna alisema kuwa pamoja na juhudi za serikali katika kuimarisha maadili, bado kuna changamoto zinazowakumba viongozi wa umma.

 

Amezitaja changamoto hizo kuwa ni pamoja na mgongano wa maslahi, matumizi mabaya ya madaraka, ushawishi wa kisiasa katika maamuzi ya kiutawala, na udhaifu wa mifumo ya usimamizi.

 

“Nitoe rai kwa kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa mifumo yetu ya uwajibikaji inaendelea kuimarishwa ili kuondoa changamoto hizi,” alisema.

Awali, Makamu Mkuu wa Chuo cha IAA Dkt. Grace Idinga alisema kuwa  makubalianao yaliyozinduliwa leo, yanalenga maeneo matatu. Ameyataja maeneo hayo kuwa ni Kuimarisha uwezo wa viongozi na watumishi wa umma kuhusu maadili, ushauri, utafiti na Ushirikiano katika Utekelezaji wa Makubaliano.

“Ushirikiano wetu utaleta manufaa makubwa kwa taifa letu, ikiwemo kuimarisha utawala bora na maadili na kuboresha utoaji wa huduma kwa umma,”alisema.

Aidha, makubaliano hayo yaliyozinduliwa leo, yatachangia kujenga utumishi katika sekta ya umma na binafsi unaoongozwa na uadilifu, uwazi na uwajibikaji.

 

 

 

 

 

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >