JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Waziri Simbachawene aigaziza Sekretarieti ya Maadili Kutumia mifumo ya kielektroniki.
29 Aug, 2023
Waziri Simbachawene aigaziza Sekretarieti ya Maadili Kutumia mifumo ya kielektroniki.

Mhe. George Simbachawene (Mb) Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ameiagiza Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kupokea matamko ya rasilimali, maslahi na madeni ya Viongozi wa Umma ili kuongeza uwazi katika utendaji kazi.

Mhe. Simbachawene ametoa agizo hilo tarehe 5 Julai, 2023 alipotembelea Ofisi za Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma zilizoko Kilimani, jijini Dodoma.

Katika ziara hiyo Mhe. Waziri aliambatana na Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb), Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

“Angalieni matumizi ya mifumo ya TEHAMA katika kupokea matamko ya raslimali, maslahi na madeni ya Viongozi wa Umma, hii itasaidia kuongeza urahisi wa viongozi kuwajibika, uwazi na kupunguza minongono katika umiliki wa mali kwa viongozi wa umma,” amesema.

Kwa mujibu wa Mhe. Simbachawene, matumizi ya TEHAMA yanayokusudiwa yanatakiwa kufungua milango kwa kiongozi wa umma kuongeza raslimali zake wakati wowote bila kusubiri mwisho wa mwaka.

“Katika matumizi ya mifumo, hakikisheni mnawashirikisha watumiaji kwasababu wao ndio wanaojua changamoto za ujazaji wa tamko,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora amesema, muundo wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma unatakiwa kuangaliwa upya ili kuiboresha na kuleta ufanisi katika utendaji kazi.

“Haiwezekani chombo kama hiki chenye historia kubwa kisiboreshwe mara kwa mara ili kuleta ufanisi katika kusimamia maadili ya viongozi wa umma,” amesema na kuongeza kuwa “Iangalieni upya miundo yenu ukama inaleta tija.”

Kwa upande wake Mhe. Ridhiwani amewataka watumishi wa Sekretarieti ya Maadili kutovunjika moyo wakati wanapotekeleza majukumu yao.

“Naipongeza taasisi yenu kwa kazi nzuri na ngumu inayohitaji busara ya kusimamia maadili ya viongozi wa umma. Napenda kuwatia moyo katika utekelezaji wa kazi zenu,’ amesema.

Naye Mhe. Jaji (Mst.) Sivangilwa Mwangesi, Kamishna wa maadili alimueleza Waziri kuwa changamoto kubwa ya Sekretarieti ya Maadili kwa sasa ni kutokamilika kwa ujenzi wa jengo la makao Makuu na Ofisi ya Kanda ya Kati ambao umetumia muda mrefu.

“Mhe. Waziri ujenzi wa jengo letu umetumia muda mrefu sana, kutokamilika kwa jengo letu kunatulazimu kuendelea kufanyia kazi katika jengo la kupanga. Kama jengo letu lingekamilika kwa wakati tungeweza kuokoa fedha za pango kutekeleza majukumu mengine.”

Mradi wa jengo la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma unasimamiwa na Wakala wa Majengo nchini (TBA).

Waziri Simbachawene amewaagiza TBA kuhakikisha wanakamilisha mradi huo kwa wakati.

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >