JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

WAZIRI MKUU: MTANZANIA USIKUBALI KUTOA RUSHWA
10 Dec, 2023
WAZIRI MKUU: MTANZANIA USIKUBALI KUTOA RUSHWA

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa amewataka watanzania wasikubali kutoa rushwa mahali popote huku akisisitiza kuwa wananchi ni wadau muhimu sana katika mapambano dhidi ya vita hiyo.

“Ninyi ni wadau wakubwa wa kukomesha rushwa, Nyie ni wadau wakubwa wa kukomesha vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu. Ili nchi yetu isiwe na vitendo vya rushwa na ukiukwaji wa haki za binadamu, wananchi mnapaswa kufichua vitendo vya ukosefu wa maadili na uvunjifu wa haki za binadamu,” alisema.

“Mtanzania usikubali kutoa rushwa popote, hasa kwenye maeneo unayopaswa kupewa huduma hiyo. wewe ni mtanzania unalindwa na sheria za nchi za kupata huduma bure kama vile hospitali bila kutoa rushwa. Inatakiwa kila Mtanzania abebe jukumu hili kwa mikono miwili, alisimamie na alitekeleze,” alisisitiza.

Aidha Mhe. Waziri Mkuu alitoa wito huo  wakati akizungumza  katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu yaliyofanyika katika viwanja vya  Nyerere Square, jijini Dodoma tarehe 10  Disemba 2023.

 

Waziri Mkuu ambaye amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. Samia Suluhu Hassan, alisema kuwa Mheshimiwa Rais amesisitiza umuhimu wa kila mmoja kuendelea kushiriki katika mapambano dhidi ya rushwa na vitendo vingine vya ukiukwaji wa haki za binadamu. Maadhimisho ya mwaka huu yamebebwa na kaulimbiu isemayo:“Zingatia Maadili, Utu, Uhuru na Haki kwa Maendeleo Endelevu.”

Mhe.Waziri Mkuu aliendelea kusema kuwa  kaulimbiu hiyo inachagiza masuala ya msingi yanayohusu maendeleo endelevu kutokana na ukweli kwamba kizazi huru chenye uadilifu, utu na kinazingatia haki ni msingi wa maendeleo ya Taifa lolote.

“Hivyo basi, hatuna budi wananchi wote kuunganisha nguvu katika ujenzi wa kizazi chenye misingi ya maadili. Kaulimbiu hii ni wito kwa sekta ya umma na sekta binafsi kutimiza wajibu wake kuhusu masuala ya maadili, utu, uhuru na haki. Kwa maneno mengine kaulimbiu hii imegusa taasisi zote na inasisitiza uwajibikaji wa kila mmoja wetu.”

Siku ya Maadili na Haki za Binadamu hapa nchini ilianza kuadhimishwa kwa pamoja mwaka 2016 ikiwa ni muunganiko wa siku mbili yaani siku ya Maadili na Haki za Binadamu.

Maadhimisho hayo huratibiwa na taasisi zinazosimamia utawala bora ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Rais Ikulu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Sekretarieti ya Maadili ya  Viongozi wa Umma, Wizara ya Katiba na Sheria, Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa, Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi, Tume ya Utumishi wa Umma, Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi, Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali pamoja na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >