JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

PO-ETHICS SECRETARIAT Logo
Viongozi Tanesco wafurahia mafunzo ya maadili na uadilifu
10 May, 2026
Viongozi Tanesco wafurahia mafunzo ya maadili na uadilifu

Viongozi kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ambao ni Mameneja wa Wilaya wamepongeza na kushukuru kwa kupatiwa mafunzo kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Viongozi hao wameyasema hayo katika mafunzo ya maadili na uadilifu kwa Viongozi wa Umma yaliyofanyika  tarehe 9 Mei, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Vizano jijini Dodoma.

Akifunga Mafunzo hayo Kaimu Mkurugenzi wa Tanesco Kanda ya Kati Mhandisi William Msome amesema kuwa uongozi bora haupimwi kwa mafanikio bali katika kufanya maamuzi sahihi kwa kuzingatia kanuni, sheria, haki pamoja na usawa.

“Kupitia mafunzo haya tutakua mabalozi wazuri wa maadili na uadilifu, na tukafanye kazi kwa kufuata miongozo iliyopo na maamuzi yetu yasimamie haki na usawa ili kuleta huduma bora bila ya upendeleo kwa wananchi,” alisema.

Mhandisi Msome ameongeza kuwa wataendelea kushirikiana na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kuratibu mafunzo ya mara kwa mara ili kuendelea kuwakumbusha Viongozi na Watumishi wa Shirika hilo suala zima la maadili na uadilifu katika utendaji wao.

Kwa upande wake Mratibu Msaidizi wa mafunzo hayo kutoka Tanesco Bi. Stella Limbumba amesema kuwa mafunzo hayo yamekwenda vizuri, na imani yake kuwa washiriki watayafanya kuwa nyenzo katika utendaji wao na yeye kama sehemu ya wasimamizi kuna kitu amejifunza kupitia mafunzo hayo.

“Sio mara ya kwanza kwa Viongozi wetu kupata semina ya maadili na uadilifu, tunafanya hivi mara kwa mara ili kuwakumbusha na kuwaweka salama wakati wa kutekeleza majukumu yao, na pia ni mazuri kwa Viongozi wapya kuwasaidia katika utendaji wao mara baada ya kupata uteuzi wa kuwa Viongozi wa Umma,” alisema Bi. Stella.

Nae Meneja Tanesco Wilaya ya Uyui iliyopo mkoani Tabora Mhandisi Hamidu Saidi Juma ametoa shukrani zake kwa waratibu wa mafunzo hayo na kuongeza kuwa maarifa waliyopata ni msingi katika utendaji wao na watayatumia katika kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma bora kwa maendeleo ya Taifa.

“Kwa kweli mafunzo ni mazuri, tunawashukuru wawezeshaji wetu kwa kutoa mada zenye kueleweka na pia darasa lilikua shirikishi na elimu tuliyopata itatusaidia katika utendaji wetu ambao lengo ni kutoa huduma bora kwa wananchi na kujenga imani kwa Serikali,” alisema Mhandisi Juma.

Mafunzo hayo yaliyodumu kwa siku mbili yaliambatana na mada mbali mbali zilizowasilishwa na wawezeshaji kutoka Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kati Dodoma, ambao ni Katibu Msaidizi Bi. Jasmin Awadhi na Bw. Alfred Mboya ambaye ni Afisa wa ofisi hiyo.

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >