JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Waziri Mhagama awataka Sekretarieti ya Maadili kujikita katika kutoa Elimu kwa Viongozi wa Umma.
27 Oct, 2023
Waziri Mhagama awataka Sekretarieti ya Maadili kujikita katika kutoa Elimu kwa Viongozi wa Umma.

Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma imeaswa kujikita zaidi kutoa elimu kwa viongozi wa umma ili viongozi watii sheria bila shuruti.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama wakati alipofanya ziara ya kukagua mradi wa ujenzi wa Makao Makuu ya Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi Umma pamoja na Kanda ya Kati Dodoma tarehe 31 Machi, 2022 jijini Dodoma.

“Jukumu mlilopewa ni la kikatiba na sisi tumeona mnavyojitoa kuhakikisha maadili yanazingatiwa ipasavyo na Viongozi wa Umma.Unapoimarisha maadili ya Viongozi wa Umma unakuwa umeimarisha utawala bora”. Alisema Mhe. Mhagama.

Mhe. Mhagama aliendelea kufafanua kuwa angependa kuwekwe msisitizo katika kuwaondoa viongozi katika kukiuka maadili kwa kujikita zaidi katika kutoa elimu kuhusu maadili kwa viongozi ambao hawajui miiko ya viongozi.

“Azma ya Serikali ya Awamu ya sita inataka kila raia wa nchi hii atii sheria bila shuruti.Pia iwe ni wajibu wao kuzingatia sheria ili kufikia lengo la nchi kuwa na utawala bora”. Alisisitaza Mhe. Mhagama.

“Ingawa kuna malalamiko ya wananchi kuhusu ukiukwaji wa maadili unaofanywa na baadhi ya viongozi na nyie ni wajibu wenu kuchunguza malalamiko hayo ili kujua kama ni ya kweli”. Aliendelea kusema Mhe. Mhagama.

Kwa upande mwingine, Mhe. Mhagama aliwaasa watumishi wenyewe wa Sekretarieti ya Maadili kuwa na maadili ili kusaidia kusimamia maadili ya wengine na kuwataka kutenda haki kwa kuzingatia sheria wakati wanaposhughulikia malalamiko kwa sababu wanashughulikia maisha ya watu.

Pia, Mhe. Mhagama aliitaka Sekretarieti ya Maadili kutoa mrejesho kwa wananchi wanaolalamika kupitia mifumo iliyopo ya Serikali.

Aidha, Mhe. Mhagama aliendelea kubainisha kuwa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wameshaandaa mfumo unaoitwa ‘e-office’ na ni matumaini yake kuwa mifumo mengine katika taasisi nyingine za serikali zitajiunga na mfumo huo.

Kuhusu maendeleo ya Mradi wa ujenzi wa Makao Makuu ya Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ambao kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na Mkandarasi umefikia asilimia 50, Mhe. Mhagama alifurahishwa na hatua zilizofikiwa na ujenzi huo.

Hata hivyo Mhe. Mhagama alimtaka Mkandarasi wa Mradi huo ambaye ni Wakala wa Ujenzi Tanzania (TBA) kufanya kazi mchana na usiku ili kuharakisha ujenzi kwani Serikali inazo fedha za kutosha kukamilisha ujenzi wa jengo hilo na miradi mingine ya ujenzi wa majengo ya Serikali inayoendelea.

“Tumekubaliana hapa hakutakuwa na muda wa nyongeza kukamilisha mradi huu kwa sababu eneo gumu la kusimamsha ‘structure’ ya jengo tayari kilichobaki ni kuweka fremu, magrili na vitu vingine vidogovidogo na kuwataka kuzingatia ubora na thamani ya fedha za umma ambazo serikali imewekeza hapa” alimaliza kusema Mhe. Mhagama.

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >