Waziri Kabudi; Viongozi wa Umma jiepusheni na mgongano wa maslahi
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Ikulu (Kazi Maalum) Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) amewaasa viongozi kuzingatia Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kuepuka mgongano wa maslah katika utendaji kazi wao.
Mhe. Kabudi amesema hayo tarehe 20.02.2026 wakati akifungua mafunzo ya maadili ya Viongozi wa Umma kwa Makatibu na Manaibu Katibu Wakuu wa Wizara yaliyofanyika katika ukumbi wa Sanaan jijini Dodoma.
“Viongozi wa Umma lazima watangulize maslah ya Umma badala ya maslah yao binafsi katika kipindi chote wanachokua madarakani hivyo, nawasihi kuzingatia maadili na kushuhulikia vyema suala la mgongano wa maslah ili kudumisha imani ya umma kwa serikali na kuaminika kwa maamuzi yanayofanywa na Serikali,”alisema.
Katika hatua nyingine Mhe.Kabudi alieleza kuwa viongozi kushindwa kutenganisha uongozi na shughuli binafsi hasa za kibiashara ni kichocheo cha kutokea mgongano kati maslah binafsi ya kiongozi wa umma na maslah ya umma jambo ambalo bado ni tatizo katika nchi yetu.
Katika hatua nyingine, Mhe. Kabudi alisema kuwa sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma haikutungwa ili kuwafanya Viongozi wawe maskini bali kudhibiti matumizi mabaya ya madaraka kwa viongozi wanaotaka kujinufaisha binafsi.
“Kiongozi kama walivyo raia wengine wa Tanzania ana haki ya kikatiba kumiliki mali na hifadhi ya mali yake kwa mujibu wa sheria. Kinachokatazwa ni Kiongozi wa Umma kutumia nafasi yake ya uongozi kujipatia mali isivyo halali,” amesema.
Mafunzo hayo yalikuwa na lengo la kukumbushana kuhusu umuhimu na wajibu wa viongozi wa umma kuzingatia maadili katika utekelezaji wa shughuli za Serikali.
“Ni muhimu kukumbushana na kubadilishana uzoefu kati ya wizara moja na nyingine kukabiliana na changamoto za kimaadili zinazojitokeza katika sekta zetu na kusababisha ubinafsi, tamaa, upendeleo na matummizi mabaya ya madaraka kwa baadhi ya watumishi wa umma ambao sio waadilifu,” amesisitiza.
Amewataka viongozi hao kujenga utumishi wa umma wenye sifa stahiki, uadilifu, uzalendo wa kitaifa, moyo wa kujituma, weledi, uwajibikaji na kufanya kazi kwa bidii kwa manufaa ya Taifa.
“Kwa nafasi za uongozi mlizonazo, umuhimu wenu katika kusimamia na kukuza maadili katika sekta ya umma hauna mjadala wala mbadala.”
Katika hatua nyingine, Waziri Kabudi ameipongeza Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kuzingatia maelekezo ya Serikali ya kutumia mifumo ya TEHAMA kutoa huduma hasa Mfumo wa Ujazaji wa tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya Mtandao (Online Declaration System - ODS).
Kwa mujibu wa Mhe. Kabudi ODS imewasaidia viongozi wengi wa umma kujaza tamko wakiwa mahali popote penye huduma ya mtandao ndani au nje ya nchi.
“Kwa matumizi ya ODS, sidhani kama kuna kiongozi ambaye ana tashwishi kujaza tamko la Rasilimali na Madeni kwa mujibu wa sheria. Viongozi wa umma ambao hawajajaza au wamechelewa kujaza tamko watakuwa na sababu zao binafsi zaidi kuliko sababu za kimfumo,” amesema.
Awali, Kamishna wa Maadili Mhe.Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi alieleza kuwa mafunzo hayo ni moja kati ya majukumu ya Sekretarieti ya Maadili kutoa elimu kwa viongozi wa umma kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
“Kupitia mafunzo haya, viongozi wanakumbushwa mambo wanayotakiwa kuzingatia wanapotimiza wajibu wao,” amesema.
Jumla ya mada mbili ziliwasilishwa katika mafunzo hayo ambazo ni mada kuhusu Changamoto za Kimaadili na nafasi ya watendaji wakuu wa Wizara kusimamia uadilifu katika sekta ya Umma na mada kuhusu udhibiti wa Mgongano wa Maslahi na uwajibikaji wa Viongozi wa umma kujenga utamaduni wa kimaadili Serikalini.
