Wazazi, Walezi na Walimu watakiwa kukemea vitendo vya ukatili kwa Watoto Nchini
Wazazi, walezi na walimu nchini wametakiwa kukemea vitendo vya ukatili kwa watoto kwa kuwatunza na kuwalinda watoto kwa kuwapatia chakula, malezi bora. Muda wa kuzungumza nao na kuwaelekeza ikiwa ni pamoja na kusimamia matumizi ya simu, mitandao ya kijamii na kushiriki kikamilifu katika mikutano ya shule, vikao vya wazazi pamoja na programu za malezi nchini.
Wito huo umetolewa na Bw. Hamad Kaaya Katibu Tawala wa Wilaya kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Hanang Mhe. Almishi Hazali alipokuwa akifungua Mdahalo kuhusu changamoto za kimaadili kwa wanafunzi na ufumbuzi wake uliofanyika tarehe 5 Disemba, 2025 katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang.
Aidha Bw. Kaaya katika hotuba yake amezitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na watoto wa shule kubakwa na wazazi na kumaliza kesi hizo nje ya mfumo pamoja na kukosa msaada rasmi wa sheria, watoto kutopata chakula cha mchana mashuleni, migogoro ya kifamilia, ulevi na wazazi kutengana, matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii jambo linalopelekea watoto kupotoshwa na maudhui ya ngono, ukatili, utapeli matusi na tabia zisizofaa.
Ameongeza kuwa changamoto nyingine zinazowakumba watoto ikiwa ni pamoja na ushawishi hasi wa makundi rika jambo linalopelekea watoto kuingizwa katika tabia kama utoro, uvutaji sigara, ulevi, na umalaya kwa watoto wa kike na changamoto nyingine ni pamoja na kukosekana kwa muda wazazi kujihusisha na malezi ya watoto wao
Aidha Bw. Kaaya amebainisha hatua za msingi zinazopaswa kuchukuliwa ili kuboresha maadili na kulinda watoto ikiwa ni pamoja na kuweka mkakati madhubuti wa kuripoti matukio ya ukatili na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria, kuzuia wazazi kumaliza kesi nje ya mfumo wa sheria. Kuimarisha ulinzi wa watoto mashuleni na katika jamii, kuzuia matumizi mabaya ya mitandao pamoja na kutoa elimu ya malezi bora kwa jamii.
Naye Katibu Msaidizi Sekreetarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya kaskazini Arusha Bw. Gerald Mwaitebele alitoa wito kwa wazazi, walezi na waalimu nchini kuhakikisha kuwa watoto wanasimamiwa kikamilifu ili kupambana na ukatili kwa watoto unaofanywa na watu wasiowaadilifu.
Kongamano hilo limefanyika ikiwa ni kuelekea kilele cha Maadhimisho ya siku ya Maadili na Haki za Binadamu Duniani ambayo hufanyika kila mwaka tarehe 10 Disemba.