Watumishi wa Maadili waaswa kuwa waadilifu.

Watumishi wa Maadili waaswa kuwa waadilifu.
Watumishi waOfisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma wametakiwa kuyazingatia na kuyaishi yote yaliyopo katika kiapo cha Ahadi ya Uadillifu kwa Viongozi na Watumishi wa Umma .
Hayo yalisemwa na Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji wa Rufani Sivangilwa Mwangesimara baada ya kuongoza kiapo cha Ahadi ya Uadilifu kwa Viongozi wa Umma na Ahadi ya Uadilifu kwa Watumishi wa Umma kwa baadhi ya watumishi wa Sekretarieti ya Maadili. Tukio hilo lilifanyika tarehe 14 Septemba 2021 katika Ukumbi wa Ofisi hiyo Jijini Dodoma.
“Nawasii katika utekelezaji wenu wa majukumu kuyaishi mliyoapa katika Ahadi ya Uadilifu,” alisema.
Ahadi ya Uadilifu ni tamko rasmi na bayana la kimaandishi linalotolewa na Viongozi wa Umma, Watumishi wa Umma na Sekta binafsi kuonesha dhamira ya kuzingatia misingi ya maadili na Mapambano Dhidi ya Rushwa.
Mhe. Kamishna aliwaasa Watumishi hao kufanya kazi kwa Uadilifu, Uwajibikaji, weledi, uzalendo na kuepuka mgongano wa maslahi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku kama walivyoahidi kwenye kiapo chao.
Jumla ya watumishikumi na sita waliohamia Sekretarieti ya Maadili hivi karibuni wameapa kiapo cha Ahadi ya Uadilifu Ikiwa ni Ishara ya Uadilifu na Uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya watumishi wa Umma.