WANACHUO WAMETAKIWA KUJIFUNZA UTUNZAJI WA MAZINGIRA NA BIASHARA YA HEWA UKAA
Wanachuo wa klabu za maadili nchini ambao pia ni wanachama wa Klabu za Maadili wametakiwa kujifunza biashara ya hewa ya ukaa na kutafsiri kibiashara kwani inaweza kuwa mkombozi mkubwa wa uchumi kwa mtu binafsi pamoja na Taifa kwa ujumla.
Wito huo umetolewa na Mkuu wa wilaya ya Dodoma, Mhe. Jabir Shekimweri wakati wa uzinduzi wa bustani ya maadili iliyopo karibu na Chuo cha Biashara CBE kilichopo jijini Dodoma tarehe 27 Februari 2026.
Aidha Mhe. Shekimweri amesema katika dunia ya hewa ukaa ukifanikiwa kusajili ekari zako kuanzia moja na ukapanda miti ya aina yoyote ile, dunia ina teknolojia ya kujua pale unazalisha hewa kwa kiasi gani na wanakulipa fedha nzuri ambayo inaweza kukutoa kwenye umasikini na ukawa bilionea.
“Tujifunze biashara ya hewa ukaa kuna wengine hapa tumetoka vijijini tunaweza kupata ata ekari moja au zaidi tukazisajili na kupanda miti baada ya miaka mitatu au zaidi inawezekana baada ya kumaliza chuo ikawa msaada mkubwa kiuchumi,” Mhe, Shekimweri.
Katika hatua nyingine Kamisha wa Maadili, Mhe. Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi amesema leo hatupandi mti tu bali tunapanda maadili, uwajibikaji na uongozi bora kwani uongozi bora haupimwi kwa maneno mazuri tu bali kwa vitendo vinavyoleta manufaa katika jamii.
“Sekretarieti ya Maadili inaunga mkono juhudi za Serikali ya kuifanya Dodoma kuwa ya kijani kwa kuzipa ushirikiano klabu za maadili kwa kutunza mazingira,” amesema.
Mhe. Mwangesi alibainisha kuwa wanachama wa Klabu za Maadili wanatakiwa kuwa mabalozi wa kesho, kwani mti ambao mtapanda leo ni ahadi ambayo mnaitoa kwa taifa lenu kwamba mtakuwa viongozi ambao mnaojali, kuwajibika na kulinda rasilimali za umma.
“Tusipande miti kwa ajili ya picha ya leo bali tupande miti kwa ajili ya kivuli cha kesho,” Mhe. Mwangesi alisisitiza.
Naye Mstahiki Meya wa jiji la Dodoma, Mhe. Alimwoni Chaula amesema Jiji la Dodoma ndio mmiliki wa eneo la bustani ya maadili lakini wameamua kulitoa kwa Sekretarieti ya Maadili kwa ajili ya kutunza mazingira na kuifanya Dodoma iwe ya kijani, eneo hili liko mjini na thamani yake kwa sasa ni zaidi ya shilingi za Kitanzania Bilioni 10 lakini jiji tumetoa kipaombele cha kutunza mazingira.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Klabu ya Maadili wa Chuo cha CBE, Ndg. Kimu Kambona ameishukuru Sekretarieti ya Maadili kwa alama ambayo wameweka kwenye Chuo chao kwa kuanzisha bustani ya maadili iliyopo jirani na chuo chao.
Aidha Mwenyekiti wa klabu ya maadili wa Chuo cha Mipango Ndg. Libwanga Kizota amefafanua kuwa wanachama wake wa Mipango watachukua jukumu la kuhakikisha sehemu hiyo inakuwa safi na ya kuvutia.
Hafla hiyo imeudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Dodoma pamoja na wanachama wa Kbalu za Maadili kutoka Chuo cha CBE, Chuo cha Mipango na Chuo Kikuu cha Mtakatifu John.
