WAMILIKI WA VYOMBO VYA HABARI NCHINI WATAKIWA KUWA MABALOZI WAZURI KATIKA KUKUZA MAADILI NCHINI.
Wamiliki wa vyombo vya habari nchini wametakiwa kuwa mabalozi wazuri katika jitihada za kukuza na kuimarisha Maadili ya Viongozi wa Umma nchini kupitia vyombo mbali mbali vya Habari kama vile Redio, magazeti, Luninga pamoja na mitandao ya kijamii.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu msaidizi sekretarieti ya maadili ya viongozi wa umma Kanda ya Magharibi Tabora Bibi Anna Mbasha alipokuwa akifungua kikao kazi kuhusu mchango wa vyombo vya habari katika kukuza Maadili nchini, kilichofanyika katika Hoteli ya JM mkoani Tabora tarehe 30 Machi 2026.
Bibi Mbasha amebainisha kuwa vyombo vya habari vina mchango Mkubwa katika jitihada za kukuza na kudumisha Maadili ya Viongozi wa Umma nchini katika kuhakikisha kuwa Maadili ya viongozi waUmma yanaimarika kwa kuelimisha na kuhabarisha umma kuhusu umuhimu wa Maadili kupitia vyombo mbalimbali vya habari nchini.
Aidha Bibi Mbasha katika hotuba yake amebainisha kuwa lengo la kikao hicho pamoja na mambo mengine ni kuongeza hamasa ya wanahabari kushiriki kikamilifu katika kukuza maadili ya viongozi wa Umma nchini pamoja na kutambua nafasi ya vyombo vya habari katika kuelimisha umma na kudumisha ushirikiano baina ya vyombo vya habari na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
”Jukumu la ukuzaji wa Maadili ya viongoziwa umma ni letu sote na linalenga kuongeza uelewa wa viongozi wa umma na wananchi kwa ujumla wake
Hivyo vyombo vya habari vina jukumu la kutoa taarifa kuhusu ukiukwaji wa wa Maadili ya viongozi pale yanapojitokeza katika maeneo mbali mbali nchini amesema”
Awali akitoa neno la utangulizi kuhusu lengo la kikao hicho Mkurugenzi wa Mipango na Tathimini kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma makao makuu Bw. Omary Juma ameeleza baadhi ya majukumu ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ambayo ni pamoja na kupokea matamko ya viongozi wa umma kuhusu Raslimali na Madeni yanayotolewa na viongozi wa umma kwa mujibu wa sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Ametaja jukumu lingine la msingi kuwa ni kufanya uchunguzi wa kina wa malalamiko na taarifa za ukiukwaji wa maadili kwa mujibu wa sheria ya maadili ya viongozi wa umma kutoka kwa wananchi.
Bwana Juma pia amewataka wamiliki wa vyombo vya habari nchini kutumia kikao kicho muhimu kujenga mahusiano mema na Sekretarieti ya Maadili ya viongozi wa Umma na pia kutoa ushirikiano mwema katika kuhabarisha Umma katika kuhakikisha masuala ya maadili yanapewa kipaumbele kupitia vyombo mbalimbali vya habari nchini.
Kikao hiki kimewashirikisha wamiliki wa vyombo vya habari nchini kutoka katika kanda ya Magharibi kutoka katika mikoa ya Shinyanga,Kigoma,Simiyu na Tabora.
