Walezi wa Klabu za Maadili wapatiwa mafunzo ya Maadili
Walezi wa klabu za Maadili ambao ni walimu kutoka shule za msingi , sekondari na vyuo katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi wamepatiwa mafunzo kuhusu maadili na namna ya kuanzisha na kuendeleza klabu za maadili.
Mafunzo hayo yaliyoratibiwa na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kaskazini-Arusha yalifanyika tarehe 27 Februari, 2026 katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro.
Akifungua mafunzo hayo Afisa Elimu Mkoa wa Kilimanjaro Bw. Abel Ntupwa alisema kuwa mafunzo hayo kwa walimu walezi wa klabu za maadili ni muhimu kwa sababu mwalimu ndio mlezi mkuu wa wanafunzi anapokua shuleni.
“Kuwepo kwa klabu za maadili katika Taasisi za elimu ni jambo zuri kwani huongeza uadilifu, kupunguza changamoto ya utoro, huongeza kasi ya ufaulu na huchochea mwenendo mwema kwani wahenga walisema mtoto umleavyo ndivyo akuavyo,” alisema.
Aidha Bw. Ntupwa alieleza kuwa upo umuhimu mkubwa wa walimu walezi wa klabu hizo kupatiwa mafunzo ya mara kwa mara kwani itasaidia katika kujenga kizazi chenye misingi imara ya maadili na kupata Taifa lenye Viongozi bora.
“Semina hii ni muhimu na tunaomba ndugu zetu wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kutukumbuka tena hapo baadae maana ni imani yangu mafunzo haya yatakua chachu ya kuwaongezea ujuzi kwa namna ya kuzifungua na kuziendeleza klabu hizi mkoani kwetu,” alisema.
Awali akitoa neno la utangulizi Katibu Msaidizi Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kaskazini –Arusha Bw. Gerald Mwaitebele alieleza kuwa jukumu kubwa wao kama Taasisi ni kusimamia na kukuza Maadili ya Viongozi wa Umma nchini hivyo wanaanza kuwaandaa mapema Viongozi wenye maadili.
“Kama chombo chenye wajibu wa kusimamia na kukuza maadili nchini tumeamua kwa dhati kabisa kuanzisha klabu za maadili katika shule za Msingi, Sekondari na Vyuo vya Elimu kwa lengo la kusimamia maadili katika ngazi ya chini kama usemi usemao samaki mkunje angali mbichi, “alisema.
Katika mafunzo hayo mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwa ni pamoja na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, majukumu ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma , misingi ya maadili katika utumishi wa umma pamoja na mada kuhusu mwongozo wa ufunguaji na uendeshaji wa Klabu za maadili.
