WAKUU WA VITENGO VYA MANUNUZI NCHINI WATAKWA KUJIEPUSHA NA VITENDO VINAVYOASHIRIA UWEPO WA MGONGANO WA MASLAHI
Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ununuzi na Ugavi wa Taasisi za Umma nchini wametakiwa kuzingatia viwango vya maadili vinavyotambulika katika utaratibu wa ununuzi wa umma nchini, vinavyosisitiza Uadilifu, Usawa, Uaminifu, kuheshimu sheria, uwazi na kuepuka Mgongano wa Maslahi.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Idara ya Ukuzaji wa Maadili Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Bw. Waziri Kipacha alipokuwa akifungua mafunzo kuhusu maadili kwa wakuu wa Idara/Vitengo vya Ununuzi yaliyofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Hoteli ya SAANAN jijini Dodoma.
Bw. Kipacha katika hotuba yake amebainisha kuwa ununuzi wa umma ndio njia ambayo Serikali inatumia kupata bidhaa na huduma zinazohitajika nchini na kwamba sehemu kubwa ya Bajeti ya Serikali inatumika katika ununuzi wa bidhaa na huduma.
Ameongeza kuwa nchini Tanzania sehemu kubwa ya bajeti ya serikali hutumiwa katika ununuzi wa bidhaa na huduma za umma, hivyo ununuzi wa umma ni mfumo ambao uko katika hatari ya rushwa na kwamba hatari ya vitendo visivyo vya kimaadili katika mchakato wa ununuzi ni kubwa ambayo inahitaji mikakati mahususi ya kuidhibiti.
“Pamoja na kuwepo kwa Sheria, Kanuni na miongozo kuhusiana na ununuzi wa Umma Maadili binafsi ni muhimu katika kuhakikisha ununuzi wa umma kimaadili” amesema.
Aidha amefafanua kuwa kuonekana kwa thamani ya fedha za Serikali katika ununuzi wa umma kunaanzia katika mchakato na taratibu za ununuzi zilivyofanyika na makosa yoyote ambayo ni kinyume na Maadili katika kusimamia mchakato huo kunasababisha upatikanaji wa bidhaa na huduma hafifu kutoka kwa Wazabuni na kutopatikana kwa thamani halisi ya fedha kutokana na ununuzi uliofanyika na hivyo kutia serikali hasara ambayo italazisha serikali kutumia fedha nyingine kwa ajili ya kupata bidhaa au huduma hiyo tena jambo ambalo ni kinyume na Maadili.
Awali akitoa neno la ufunguzi, Katibu Msaidizi, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Bi. Sigolwike Mkamati alisema kuwa lengo la mafunzo haya ni kuwakumbusha viongozi wa umma kuhusu masuala ya kimaadili ya kuzingatiwa katika utekelezaji wa shughuli za Serikali.
Bi. Mkamati ameyataja baadhi ya malengo hayo kuwa ni pamoja na kusisitiza umuhimu wa kuzingatia maadili ya uongozi ili kudumisha imani ya wananchi kuhusu uwajibikaji wa viongozi wa umma na utaratibu wa kutoa maamuzi serikalini.
Amesema lengo lingine ni kuhimiza masuala yanayohusu mgongano wa maslahi na namna ya kudhibiti ili kulinda maslahi ya umma na pia kukumbushana kuhusu taratibu za Ujazaji wa Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya Mtandao (ODS).
Jumla ya mada tatu (3) zimejadiliwa katika mafunzo hayo ambazo ni udhibiti wa Mgongano wa Maslahi katika Ununuzi wa Umma nchini, changamoo za kimaadili na wajibu wa Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ununuzi wa Umma kudumisha uadilifu katika mchakato wa ununuzi na Mada ya mwisho ni Mfumo na Ujazaji wa Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya Mtandao (Online Declaration System (ODS.)
