JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

PO-ETHICS SECRETARIAT Logo
Wakuu wa Vitengo na Idara za TEHAMA wajengewa uwezo matumizi ya ODS
03 Mar, 2026
Wakuu wa Vitengo na Idara za TEHAMA wajengewa uwezo  matumizi ya ODS

Wakuu wa Vitengo na Idara za TEHAMA kutoka Taasisi za Umma na Wizara  nchini wametakiwa kuwa msaada kwa kuwaelekeza Viongozi wengine katika Taasisi zao namna ya matumizi ya mfumo wa ujazaji Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya Mtandao (Online Declaration System-ODS).

Rai hiyo imetolewa na Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kati-Dodoma Bi. Jasmin Awadhi wakati akifungua mafunzo ya maadili kwa Wakuu wa Vitengo na Idara za TEHAMA kutoka Taasisi za Umma na Wizara yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Bodi ya Usajili wa Makandarasi jijini Dodoma tarehe 03 Machi, 2026.

“Lengo la mafunzo haya ni kuwapitisha katika matumizi ya mfumo wa ujazaji Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya Mtandao na baada ya kupata uelewa wa mfumo huu tunatarajia mtakua msaada kwa wengine katika kujaza  Tamko,”alisema.

Aidha Bi. Jasmin ameongeza kuwa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma haijakataza Kiongozi kumiliki mali, bali ni nyenzo katika kuhakikisha kuwa Viongozi wa Umma wanapata mali zao kwa njia halali kwa kuepuka matumizi mabaya ya madaraka na magongano wa maslahi.

“Sheria hii haimzui mtu kuwa na mali kwa kadri alivyojaliwa ila katika kulinda taswira ya Kiongozi na Serikali kwa ujumla, Kiongozi lazima atafute mali zake kwa njia sahihi na kisha kuzitamka kwa mujibu wa Sheria,” alisisitiza Bi. Jasmin.

Awali akitoa mada kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Afisa Maadili kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kati-Dodoma Bw. Anno Mgani amesema kuwa Kiongozi mzuri ni yule anayefanya kazi kwa kuzingatia weledi, mwenye kuepuka kuomba au kupokea fadhila yoyote ya kiuchumi na mwenye kutoa huduma bila upendeleo.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA kutoka Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini Bw. Jabir Saleh Abdi amesema kuwa mafunzo hayo ni mazuri kwani matumizi ya mfumo wa ODS yameondoa matumizi ya karatasi ngumu ambapo gharama kubwa ilikua ikitumika katika kujaza na kuwasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni kwa Kamishna wa Maadili.

“Mfumo umeleta nafuu katika kujaza taarifa zetu, kwani unafanya kazi popote penye huduma ya mtandao, hivyo ni rahisi kwetu kujaza Tamko tukiwa ofisini bila kuathiri utekelezaji wa majukumu yetu ya kila siku,” alisema Bw. Abdi.

Mafunzo hayo yaliyowashirikisha Wakuu wa Vitengo na Idara za TEHAMA kutoka Taasisi za Umma na Wizara yalikua na lengo la kuwajengea uwezo Viongozi hao katika matumizi ya mfumo kwenye kujaza Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya Mtandao (Online Declaration System-ODS) na wao kutakiwa kuwa mabalozi wazuri wa mfumo huo kwa Viongozi wengine katika maeneo yao ya kazi.

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >