Waandishi wa vyombo vya habari waaswa kutumia kalam zao vyema.
Wahariri na waandishi wa vyombo vya habari wameaswa kutumia kalamu zao vyema wakati wa kuandaa na kuripoti baadhi ya matukio mbalimbali ili kukuza uadilifu nchini na kuleta Imani ya wananchi kwa viongozi wao na serikali kwa ujumla.
Hayo yalisemwa na Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kanda ya Mashariki - Morogoro Bw, Hendry Sawe alipokua akifungua mafunzo ya maadili kwa wahariri na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari kutoka mkoani Morogoro.Mafunzo hayo yalifanyika katika ukumbi wa Hazina Ndogo mkoani Morogoro tarehe 08 Aprili,2026
Bw. Sawe alisema kuwa ni vyema waandishi wa habari wakaandika habari ambazo zina tija kwa wananchi kwani kile wananchi wanacholishwa kuhusu viongozi wao ndicho wanachokiamini “Niwaombe mkatumie kalamu zenu vyema katika kuhabarisha umma na kufichua matendo yasiyo ya kimaadili kwa Viongozi wa Umma”alisema.
Bw, Hendry Sawe alisema kuwa Taasisi imeona vyema kutoa mafunzo ya maadili kwa wanahabari hao ikiwa na lengo la kuimarisha mashirikiano kati ya Taasisi kama msimamizi wa maadili na vyombo vya habari kama mdau muhimu wa ukuzaji wa maadili.
“Tumeandaa mafunzo haya mahsusi kwa wahariri na waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari kwa sababu tunajua vyombo hivi ni wadau wakubwa wa ukuzaji wa maadili hivyo tumekuja kujadiliana namna gani tunaweza kukuza hali ya maadili ya Viongozi wa Umma nchini”alisema.
Naye Msimamizi wa ITV media mkoa wa Morogoro Bi. Idda Mushi alisema kuwa mafunzo hayo yatakua manufaa makubwa kwa waandishi wa habari katika kuandaa na kuandika habari mbalimbali “Sote ni mashahidi hatujatoka patupu tumeelimishwa kuhusu mambo mbalimbali ya kimaadili ambayo mengi tulikua hatuyafahamu kwa hiyo niwasihi wenzangu tukitoka hapa tukaandae Makala, habari mbalimbali za kimaadili zenye faida kwa jamii kwa ujumla” alisema.
Bi. Idda alisisitiza suala zima la waandishi kuwa wazalendo katika utekelezaji wa majukumu yao ya uandishi kwani kukosa uzalendo kwa mwandishi kunaweza kuiathiri nchi .“Ndugu zangu niwakumbushe kuwa Tanzania ni moja na ni yetu sote hakuna mtu atakayetoka nje na kuja kuijenga kwa hiyo kila tunachokifanya tuwe wazalendo na nchi yetu tukitumia vibaya kalamu zetu tunaweza kuharibu badala ya kuijenga nchi yetu kama ambayo tumekusudia” alisema.
Mada mbili ziliwasilishwa katika mafunzo hayo ambayo ni mada kuhusu Sheria ya Maadili pamoja na mada kuhusu majukumu ya Sekretarieti ya Maadili.
