Vyombo vya habari vyatajwa nguzo muhimu katika kukuza na kuimarisha maadili nchini
Vyombo vya habari nchini vimetajwa kuwa nguzo muhimu katika kukuza na kuimarisha maadili kwa Viongozi wa Umma na Taifa kwa ujumla.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum Bi. Elizabeth Komba wakati akifungua kikao kazi na wadau wa habari wa Kanda hiyo ambao ni wamiliki, wahariri na waandishi wa habari kwa lengo la kujenga ushirikiano endelevu kati ya Taasisi hiyo na vyombo vya habari nchini.
Kikao kazi hicho kimefanyika katika ukumbi wa mikutano wa Shule ya Uongozi Mwalimu Nyerere mjini Kibaha mkoani Pwani tarehe 9 Aprili, 2026.
Katika hotuba yake kwa wadau hao Bi. Elizabeth alisema kuwa vyombo vya habari sio kioo tu cha jamii bali ni chombo cha kuunda na kukuza maadili nchini.
“Tunaamini kuwa vyombo vya habari vina nafasi ya kipekee katika kukuza maadili, uwajibikaji na uwazi katika jamii, kwa maneno mengine nyinyi ni nguzo muhimu katika kujenga au kubomoa maadili katika jamii, hivyo tutumie tasnia hii kujenga jamii yenye uadilifu,” alisema Bi. Elizabeth.
Aidha Bi. Elizabeth ameongeza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa katika kukuza uwajibikaji kwa kufichua vitendo vya rushwa, ubadhilifu au matumizi mabaya ya madaraka kwani vinaweka wazi ukweli ambao ni rahisi kwa muhusika kuwajibika.
“Kama tukitumia vyombo vya habari kwa njia sahihi tunaweza kujenga jamii yenye uadilifu uwazi na haki na tukivitumia vibaya tunaweza kuharibu maadili na kuleta migawanyiko miongoni mwetu na hatimaye kujenga jamii isiyokua na uzalendo,” alisisitiza.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mipango, Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Bw. Omary Juma amesema kuwa ushirikiano huo utakua endelevu na mara kwa mara watakua wanakutana kwa lengo la kufanya majadiliano kwa ajili ya kupata namna bora ya kukuza na kuimarisha maadili nchini.
