Vyombo vya habari ni daraja la kukuza Maadili ya Viongozi wa Umma.
Vyombo vya habari nchini vimetajwa kuwa daraja kati ya wananchi na Viongozi wao katika kukuza na kuimarisha maadili ya Viongozi wa Umma na serikali kwa ujumla.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Mashariki Bw. Hendry Sawe wakati akifungua kikao kazi na wadau wa habari wa mkoa wa Tanga . Wadau hao ni wamiliki, wahariri na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali mkoani Tanga.
Kikao kazi hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Bandari mkoani Tanga terehe 10 Aprili, 2026.
Katika hotuba yake kwa wadau hao Bw. Sawe alisema kuwa vyombo vya habari ni kiungo muhimu kati ya viongozi na wananchi pale vinapotekeleza wajibu wao kwa weledi na uadilifu wa hali ya juu vitachangia kwa kiasi kikubwa kujenga viongozi waadilifu na jamii yenye misingi imara ya maadili.
Katika hatua nyingine Bw. Sawe alieleza kuwa vyombo vya habari vinaweza kusaidia kukuza maadili ya viongozi kwa kuandaa Makala ama vipindi vinavyoeleza kuhusu maadili ya viongozi, kuibua na kufichua vitendo visivyo vya kimaadili kama rushwa, matumizi mabaya ya madaraka na mambo mengine kama hayo.
“Kumekua na changamoto ya Baadhi ya Vyombo vya habari kutoa habari za upotoshaji taarifa zisizo sahihi zinazosababisha kuporomoka kwa Imani ya wananchi dhidi ya Taasisi za Umma na Serikali kwa ujumla hivyo niwaombe mkatoe taarifa za ukweli na zenye takwimu sahihi zenye lengo la kuijenga nchi yetu” alisema.
Bw. Sawe alieleza kuwa lengo la kikao kazi hicho ni kujenga ushirikiano endelevu kati ya Taasisi hiyo na vyombo vya habari nchini “Kama Taasisi tumeona ni vyema kufanya kikao kazi na nyinyi ili tuweze kujadiliana ni namna gani tunaweza kukuza maadili ya Viongozi wa Umma kupitia vyombo vya habari ambavyo ndio daraja kati ya wananchi na serikali ambayo inaongozwa na viongozi mbalimbali”alisema.
Naye Bi. Evelyn Balozi Meneja wa kituo cha redio cha Utume Fm kutoka wilayani Lushoto alisema kuwa kikao kazi hicho kimekua na manufaa makubwa kwa wanahabari hao kwani kimewapa fursa ya kuifahamu kwa kina Sekretarieti ya Maadili ikiwa ni pamoja na majukumu yake na misingi ya Viongozi wanayopaswa kuifuata ’’Kupitia kikao kazi hiki tumejifunza pia kuwa ni namna gani tunawajibika kuwa daraja kati ya Sekretarieti ya Maadili na jamii kwa kuibua matendo yasiyo ya kimaadili yanayofanywa na Viongozi pamoja na kuelimisha jamii kuhusiana na masuala ya kimaadili’’ alisema.
Mada mbili ziliwasilishwa katika kikao kazi hicho ambazo ni pamoja na mada kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma sura 398 pamoja na mada Ushirikiano wa Sekretarieti ya Maadili na vyombo vya habari.
