Viongozi wa Umma watakiwa kutenda haki wanapotekeleza majukumu yao
Wito umetolewa kwa Viongozi wa Umma kuongozwa na dhamira ya kutenda haki bila woga wanapotekeleza majukumu yao.
Wito huo umetolewa na Katibu Idara ya Ukuzaji wa Maadili kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Bw. Waziri Kipacha wakati akitoa mafunzo kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa Waheshimiwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria.
Mafunzo hayo yametolewa katika kikao kati ya Kamati hiyo na Taasisi zilizopo chini ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kilichofanyika katika ofisi za Bunge jijini Dodoma tarehe 11 na 12 Februari, 2026.
Bw. Kipacha amesema kuwa, “Viongozi wa Umma wanapotekeleza majukumu yao wanapaswa kuongozwa na dhamira ya kutekeleza majukumu kwa uadilifu, uaminifu, haki, bila woga au upendeleo ili kuongeza imani ya wananchi kwa Serikalii yao,” ameeleza.
Kwa mujibu wa Bw. Kipacha, msingi huu ukipuuzwa hupunguza imani ya wananchi kuhusu uadilifu wa Viongozi wa Umma na utaratibu mzima wa utoaji maamuzi katika Taasisi za Umma.
“Viongozi wa Umma wamepewa dhamana ya kufanya maamuzi kwa niaba ya wananchi hivyo, inawalazimu kuzingatia viwango vya juu vya maadili.”
Amezitaja baadhi ya faida za maadili kuwa ni kuelewa, kuchambua na kupambanua mambo mema na maovu, mazuri na mabaya, mambo yanayokubalika na yasiyokubalika, yanayositirika na yasiyositirika na kuamua kutenda jambo sahihi wakati wote, mahali popote hata kama hakuna mtu anayekuona.
Katika mafunzo hayo, Bw. Kipacha amewakumbusha Waheshimiwa wabunge kuwa, “iwapo Mhe. Mbunge atakiuka Ibara ya 67 (1)(d) na 71 (1)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Mungano wa Tanzania, uchaguzi Mkuu wa mwaka 2030 utakuwa haumuhusu.”
Katika kikao hicho Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala ,Katiba na Sheria ilikua chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Dkt. Damas Daniel Ndumbaro (Mb), wakati Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora iliwakilishwa na Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Regina Qwaray (Mb).
