JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

PO-ETHICS SECRETARIAT Logo
Viongozi wa Umma waaswa kuzingatia Sheria ya Maadili
06 Mar, 2026
Viongozi wa Umma waaswa kuzingatia Sheria ya Maadili

Viongozi wa Umma wameaswa kuzingatia Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma sura ya 398 wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

Wito huo umetolewa na Katibu Msaidizi  Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Mashariki-Morogoro Bw. Hendry Sawe alipofungua mafunzo ya maadili kwa Viongozi mbalimbali  wa Umma na wataalam wa masuala ya TEHAMA kutoka jijini Tanga .

Mafunzo hayo ya siku moja yalifanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Bandari  ya Tanga tarehe 05 Machi, 2026.

Bw. Sawe alieleza kuwa Kiongozi yeyote anapaswa kuishi kwa kutii Sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyowekwa na Serikali kwa  kuyaishi yale anayoapaa na kuahidi pindi anapoteuliwa ama kuchaguliwa katika nafasi za uongozi.

“Ili Kiongozi aweze kusimamia wenzake ama kukemea maovu lazima awe mfano wa kuigwa na kuishi katika utamaduni wa uadilifu na kuyafanyia kazi kwa vitendo yale aliyoapa wakati alipoteuliwa katika nafasi husika.” alisema.

Bw. Sawe alifafanua kuwa  kwa mujibu wa kifungu cha 6 cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma (sura ya398 marejeo rekebu ya 2023) kimeainisha misingi ya maadili ambayo msingi mojawapo ni kutoa Tamko la Tasilimali na Madeni kwa viongozi wa Umma .

“Kwa muktadha huo ni kuwa suala la Kiongozi kutamka mali zake lipo kisheria hivyo ni wajibu kwa Kiongozi yeyote wa Umma  kutii na kuzingatia  matakwa haya  ili kukuza Imani ya wananchi kwa serikali yao,” alisisitiza.

Katika hatua nyingine Bw. Sawe ameeleza kuwa katika kuhakikisha kuwa Viongozi wanatekeleza takwa hilo bila changamoto Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ilianzisha mfumo wa ujazaji wa Tamko la Rasilimali, Maslahi na Madeni kwa njia ya mtandao ili iwe rahisi kwa Kiongozi kufanya hivyo akiwa popote pale Ulimwenguni.

“Mtakumbuka kuwa tokea kuanzishwa kwa Taasisi hii Viongozi wamekua wakitoa matamko yao kwa njia ya makaratasi lakini sasa tumeamua kwenda kidigitali kama ambayo matamko hayo sasa yanajazwa kwa nja ya mtandao,” alisema.

Pamoja na hayo Bw. Sawe alifafanua kuwa  mfumo hu una faida nyingi kwa Viongozi  kwani kiongozi anaweza kujaza taarifa zake mahali popote alipo na kwa Taasisi unapunguza muda wa kufanya kazi na kuongeza ufanisi zaidi.

“Mfumo wetu umeunganishwa na mifumo mbalimbali mfano TRA, EGA DAWASA, TANESCO, NIDA, BREALA na mingine mingi kwahiyo ni rahisi kupata taarifa za Viongozi kwa usahihi mkubwa na kuongeza ufanisi wa zoezi hili,” alisema.

Bw. Sawe aliendelea kusema kuwa Sekretarieti imekua ikitoa mafunzo kwa Viongozi lakini imeona ni vyema kutoa   mafunzo hayo kwa  maafisa TEHAMA ili waweze kuwasaidia  Viongozi wengine katika sehemu zao za kazi.

 “Tumeamua kutoa mafunzo haya kwa wataalam wa TEHAMA kwa sababu wao wanakaa karibu na baadhi ya Viongozi mfano Wabunge,Madiwani Wakuu wa Idara nk hivyo tuna Imani watatusaidia kuwapatia elimu hii wale walengwa wetu ambao ni Viongozi na kuwapa msaada pale inapobidi”alisema.

Naye mshiriki wa Mafunzo hayo Bi. Aqwilina Kirita Mkuu wa Hazina ndogo jijini Tanga  alisema kuwa wamenufaika na mfumo huo kwani umewapunguzia gharama na muda wa kutekeleza zoezi hilo.

“Hapo nyuma tulikua tunasafiri hadi Ofisi za Kanda kuwasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni jambo lililokua linatuchukulia muda na pia kutuongezea gharama za usafiri  lakini sasa  tunajaza kwa urahisi tukiwa mahali popote,” alisema.

Mada mbili ziliwasilishwa katika mafunzo hayo ikiwa ni mada kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma pamoja na mada kuhusu Ujazaji wa Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya Mtandao.

.

 

 

 

 

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >