JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Viongozi wa Umma mkoani Kagera watakiwa kuepuka Mgongano wa Maslahi.
08 May, 2025
Viongozi wa Umma mkoani Kagera watakiwa kuepuka Mgongano wa Maslahi.

Katibu Tawala Msaidizi  Rasilimaliwatu Mkoa wa  Kagera Bw. Bwai Mashauli Biseko amewataka Viongozi wa Umma mkoani Kagera kuepuka vitendo vinavyoashiria uwepo wa mgongano wa masilahi ili kuweza kuwasimamia watumishi waliochini ya Idara zao na  kuhakikisha wanafanya kazi kwa kuzingatia weledi na maadili katika kutekeleza majukumu yao.

Bw. Biseko akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera  Mhe. Fatma Mwassa  ameyasema hayo  alipokuwa akifungua mafunzo kuhusu maadili ya Viongozi wa Umma yaliyofanyika mkoani Kagera katika ukumbi  wa mikutano wa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba tarehe 8 Mei, 2025.

Bw. Biseko amebainisha kuwa swala la mgongano wa masilahi katika utumishi wa umma limekuwa likiathiri sana ufanisi kwenye  utekelezaji wa majukumu ya Serikali ambapo baadhi ya Viongozi wasio waadilifu wamekuwa wakijiingiza kwenye mgongano wa masilahi kwa lengo la kujinufaisha wao ,familia zao,pamoja na marafiki zao.

”Jambo hili limekuwa likisababisha kasi ndogo ya ukuwaji wa uchumi pamoja na utoaji wa huduma duni kwa wananchi,” amesema.

Aidha Bw. Biseko amefafanua kuwa ili kuhakikisha  tatizo hilo linakomeshwa ni vyema elimu kuhusu Sheria ya Maadili pamoja na mgongano wa Maslahi iwe inatolewa mara kwa mara kwa Viongozi wa Umma,Watumishi wa Umma pamoja na sekta binafsi.

Katika hatua nyingine Bw. Biseko  amewataka washiriki wa mafunzo hayo ambao ni Viongozi wa Umma kutumia vyema elimu waliyopata kupitia mafunzo hayo ili kuleta mabadiliko na hatimaye kufanya kazi kwa kuzingatia  uadilifu  na nidhamu kwa maendeleo ya Taifa.

Awali akiongea na washiriki wa mafunzo hayo, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Bukoba Mhe. Godson Gupson amesema kuwa uwepo wa mgongano wa maslahi kwa Viongozi umekuwa kikwazo kikubwa katika utekelezaji wa majukumu kwa Viongozi jambo linalopelekea uwepo wa maamuzi yasiyokubalika.

“Mgongano wa Maslahi unapunguza tija katika utendaji wetu na kusababisha Serikali kutotekeleza majukumu yake kwa kiwango kinachostahili na kupoteza ufanisi wa shughuli za Serikali,” amesema.

Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo Bi.Fatina Laay ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba amesema mafunzo waliyopatiwa yatasaidia katika kukuza maadili kwa Viongozi waliyopo chini yao na kuhakikisha wanakua makini katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Mafunzo hayo yamewashirikisha Viongozi wa Umma wa Mkoa wa Kagera wakiwemo Wakurugenzi wa Halmashauri, Wakuu wa Taasisi mbalimbali pamoja na Wakuu wa Idara na Vitengo na watumishi wengine wa Umma wakiwemo Mahakimu wa Mahakama za Wilaya.

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >