JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Viongozi wa Manispaa ya Bukoba waaswa kuwa waadilifu
02 Feb, 2024
Viongozi wa Manispaa ya Bukoba waaswa kuwa waadilifu

Viongozi wa Manispaa ya Bukoba wametakiwa kuwa waadilifu, waaminifu na kuepuka migongano ya maslahi katika utendaji kazi wao ili kulinda viapo vyao.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera Dkt. Toba Nguvila alipofungua mafunzo ya Maadili kwa Viongozi wa umma wa Manispaa ya Bukoba yaliyofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera tarehe 25 Januari, 2024.

Dkt. Nguvila aliwaeleza Viongozi hao kuwa ipo haja ya kujenga na kulinda utamaduni wa kuzingatia maadili sahihi katika taasisi wanazotumikia na kusimamia maadili kwa katika Taasisi wanazoziongoza.

”Kama mnavyofahamu suala la maadili ni nguzo muhimu sana katika jamii kwani maadili yanasaidia kudhibiti mianya ya rushwa na vitendo vingine visivyo na Maadili na kuleta amani na utulivu katika jamii jambo linalotuwezesha kufanikisha mipango ya maendeleo katika nchi yoyote ile duniani hivyo, tunapaswa kulipa kipaumbele,’’ alisema.

Kwa mujibu wa Dkt. Nguvila, suala la mgongano wa Maslahi kwa viongozi limekuwa likiathiri utendaji kazi kwa baadhi ya viongozi na kushauri elimu kuhusu Mgongano wa Maslahi itolewe kwa kiwango cha juu kabisa katika jamii yetu.

Aidha, Katibu Tawala huyo wa Mkoa wa Kagera amewataka Viongozi wa Umma kupitia mafunzo hayo kubadilika katika utendaji wa kazi na kuongeza nidhamu ya Maadili ili kujenga imani kwa wananchi wanaowaongoza pamoja na Serikali kwa ujumla.

Awali akitoa maelezo kuhusu mafunzo hayo Katibu Msaidizi Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Ziwa- Mwanza Bw. Godson Kweka alieleza kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwakumbusha Viongozi  wa Umma kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Alisema, Mafunzo hayo yalilenga kuwakumbusha Viongozi wa Umma kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuwaingiza katika mgongano wa maslahi kwani tatizo hilo ni kubwa sana na linaathiri maendeleo ya nchi.

“Viongozi na watumishi wenzangu sisi kama Taasisi inayosimamia maadili tumekuja kuwakumbusha kuwa mnaposhughulikia miradi ya serikali msiingize masuala yenu binafsi mfanye maamuzi kwa kuzingatia maslahi ya umma,” alisema.

Washiriki wa mafunzo hayo ya siku moja walikuwa Kamati ya Usalama ya mkoa wa Kagera, Viongozi wa Mahakama, Wakuu wa Taasisi, Wakuu wa Idara na Vitengo Sekretarieti ya Mkoa, Madiwani na Wakuu wa Idara na Vitengo Manispaa ya Bukoba.

Mada zilizowasilishwa ni Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Uwajibikaji wa pamoja, pamoja na Mgongano wa Maslahi.

 

 

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >