JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

VIONGOZI SITA WAFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI:
27 Mar, 2025
VIONGOZI   SITA WAFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI:

Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma imewafikisha mbele ya Baraza la Maadili Viongozi sita wa Umma kwa kushindwa kuwasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni kwa Kamishna wa Maadili kinyume cha Sheria.

Viongozi waliofikishwa mbele ya Baraza la Maadili tarehe 27 Machi, 2025 katika ukumbi wa ofisi za Sekretarieti ya Maadili ni; Mhe. Edward Mhina Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba wa wilaya ya Korogwe, mkoani Tanga, Mhe. Mwandei Mohamed, diwani halmashauri ya wilaya Mkinga, Mhe. Mussa Bohero Jangwa diwani wa kata ya Mayomboni, Tanga na Bi. Mwajuma Abas Kihiyo, Msajili wa Hati Msaidizi, Tanga.

Viongozi wengine ni Bw. Idefonce Columba, Meneja wa TANESCO wa wilaya ya Kaliua, mkoani Tabora, Mhe.  Cleopha Mziray, hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Puge, mkoani Tabora.

Wakili Mkuu wa Serikali Bi. Emma Gelani ameliambia Baraza kuwa walalamikiwa wote sita kwa pamoja wanadaiwa kushindwa kuwasilisha  Tamko la Rasilimali na Madeni kwa Kamishna wa Maadili kinyume na misingi ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Sura ya 398.

“Mhe. Mwenyekiti, kushindwa kuwasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni ni ukiukwaji wa misingi ya uongozi kwa mujibu wa kifungu cha 9(1)(b) na kifungu cha 16(a) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma,” alisema.

Viongozi hao wanatuhumiwa kushindwa kuwasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni kati ya mwaka 2021 hadi 2023.

Walalamikiwa wote katika nyakati tofauti wamekiri kosa.

Mmoja wa watuhumiwa hao Bw. Musa Jangwa alipoulizwa na Mhe. Rose Teemba, Mwenyekiti wa Baraza la Maadili kama amesikia malalamiko yake amesema, “Ndio nimeyasikia Mhe. Nakiri kosa na naliomba Baraza lako linisamehe aksante.”

“Kwa kuwa maelezo yametolewa na umekiri kwa kinywa chako, Baraza limekutia hatiani. Unaweza kwenda,” alisema Mhe. Teemba.

Baraza hili limefanyika chini ya Mwenyekiti wake Jaji (Mst.)  Rose Teemba, akisaidiana na Wajumbe wa Baraza hilo Bw. Peter Ilomo na Bi. Suzan Mlawi.

Upande wa mashtaka uliwakilishwa na Wakili Mkuu wa Serikali Bi. Emma Gelani, Bw. Hassan Mayunga, Bw. Hillary Hassan, Lydia Mwakibete na Catherine Tibasana.

Kikao hicho cha Baraza kimeahirishwa hadi tarehe 28 Machi 2025 ambapo walalamikiwa wengine watatu akiwemo Mhe. Sakina Jumanne Mohamed, Mkuu wa wilaya ya Mbogwe mkoani Geita watafikishwa mbele ya Baraza.

 

 

    

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >