VIONGOZI KANDA YA MAGHARIBI WAPIGWA MSASA SHERIA YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA
Viongozi mbalimbali wa Umma ambao ni Wakuu wa Idara/Kitengo cha TEHAMA kutoka Halmashauri za Wilaya, Manispaa na miji katika Kanda ya Magharibi wapatiwa mafunzo kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Mafunzo hayo yalifanyika katika ukumbi wa Grand Penta Hotel mkoani Tabora tarehe 12 Februari, 2026. Akifungua mafunzo hayo Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Magharibi-Tabora Bi. Anna Mbasha alisema kuwa lengo la kuratibu mafunzo hayo ni kuwakumbusha Viongozi juu ya uzingatiaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na.13 ya mwaka 1996 katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
“Viongozi wenzangu tumekuja hapa kukumbushana juu ya Sheria ya Maadili itusaidie katika utekelezaji wa majukumu yetu ya kila siku kama Viongozi kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu pamoja na kuzingatia misingi ya Maadili ya Viongozi wa Umma” alisema.
Aidha Bi. Mbasha alieleza kuwa suala la kuzingatia maadili kwa Viongozi wa Umma ni muhimu kwa sababu maadili ndio msingi wa uongozi bora na unao aminika kwa wananchi kwani sheria inawataka viongozi kufanya kazi kwa maslahi ya umma badala ya maslahi yao binafsi.
“Wananchi wanamategemeo makubwa sana kwa Serikali yao na nyinyi kama viongozi wa Halmashauri ndio watekelezaji wa mikakati yote ya Serikali msipozingatia sheria kwa kufanya maamuzi ya haki na yenye kuzingatia maslahi ya wananchi lazima mtakwaruzana na wananchi watakosa Imani na Serikali yao” alisema.
Katika hatua nyingine Bi. Mbasha alieleza kuwa katika mafunzo hayo pia Viongozi watapatiwa elimu ya namna ya utumiaji wa mfumo wa ujazaji wa Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya mtandao (ODS) “Kama tunavyojua sasa hivi Viongozi wote wanajaza Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya mtandao hivyo tumeona kuwa upo umuhimu wa kuwaelekeza namna ya matumizi sahihi ya mfumo huu ilikufanya zoezi hili kuwa rahisi na rafiki kwetu sote” alisema.
Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Maadili Afisa Maadili Bw. Patrick Shayo alieleza juu ya misingi ya maadili ya Viongozi wa Umma ambayo ni pamoja na Kujiepusha na mgongano wa maslahi, kufanya maamuzi kwa kuzingatia misingi ya sheria, kanuni na taratibu, kujiepusha na kupokea zawadi, kutoa Tamko la Rasilimali maslahi na madeni, kutenda haki, kutumia taarifa za ofisi kwa manufaa binafsi, kutoa taarifa za kiofisi kwa watu wasiohusika.
“Ni kosa la kisheria kiongozi akishindwa kuzingatia misingi ya Maadili na adhabu yake ni kwa mujibu wakifungu cha 8 cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ambazo ni pamoja na kushushwa cheo, kusimamishwa, ama kufukuzwa kazi, kushauriwa kujiuuzulu pamoja na adhabu nyingine mbalimbali” alisema.
Viongozi walioshiriki mafunzo hayo yaliyokua na lengo la kuwakumbusha masuala mazima ya uadilifu kwa Viongozi wa Umma ni Wakuu wa Idara na Kitengo cha TEHAMA kutoka Kanda ya Magharibi.
