JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

PO-ETHICS SECRETARIAT Logo
Uongozi wenye Maadili huimarisha Imani ya wananchi kwa serikali.
15 Apr, 2026
Uongozi wenye Maadili huimarisha Imani ya wananchi kwa serikali.

Uongozi wenye Maadili huimarisha Imani ya wananchi kwa Taasisi za Umma na serikali kwa ujumla. Wananchi wanapowaona Viongozi wao wakitenda kwa haki, uwazi na uadilifu huongeza ushirikiano, utii wa sheria na mshikamano katika jamii inayowazunguka.

Hayo yalisemwa na Mhe. Mathew Kirama Katibu na Mtendaji Mstaafu, Ofisi ya Rais Tume ya Utumishi wa Umma akimuwakilisha  Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi , Kamishna wa Maadili alipokua akifungua mafunzo ya maadili kwa Wakurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu, Makatibu Tawala wasaidizi wa mikoa na Makatibu Tawala wa wilaya . Mfunzo hayo yalifanyika katika ukumbi wa hoteli ya Morena-Morogoro  tarehe 15 Aprili,2026.

Katika hotuba yake Mhe. Kirama alisema kuwa katika mazingira ya sasa ya  Utumishi wa umma  maadili kwa Viongozi ni suala muhimu sana kwani kuna mtanziko mkubwa wa changamoto za kimaadili kuanzia ngazi ya familia, taasisi za umma na jamii kwa ujumla. Hivyo Viongozi wanapaswa kuwa mfano mzuri wa uzingatiaji wa maadili ili kuimarisha utawala bora na kuwa chachu ya maendeleo kwa serikali.

 “Viongozi wa Umma mnatarajiwa kuwa kielelezo kizuri cha uaminifu, uwazi, usawa na uzingatiaji wa sheria katika maamuzi yenu ya kila siku ili kujenga Imani ya wananchi kwenu na serikali yao kwa ujumla” alisema.

Mhe. Kirama  aliendelea kusema kuwa maadili si suala la hiari bali ni suala la lazima na msingi wa uongozi bora na utendaji wenye tija kwa watumishi  na Viongozi wa umma. Maadili husaidia kuzuia migongano ya maslahi, matumizi  mabaya ya madaraka, rushwa na upendeleo na mambo mengine kama hayo.

“Maadili hujenga utamaduni wa kuwajibika, huimarisha nidhamu ya kiutumishi na huogeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya  viongozi kwa umma “ alisema.    

Naye mshiriki wa mafunzo hayo Mhe. Glory Absalum, Katibu Tawala –Kahama alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu sana kwa viongozi hao kwani wao kama wasimamizi wa rasilimali za nchi  wanatakiwa kuhakikisha   kwamba wananchi wanapata huduma bora kutoka kwa serikali yao.

“Niwasihi Viongozi na watumishi wenzangu kuhudhuria mafunzo haya ambayo tumeambiwa yana muendelezo kwa mujibu wa ratiba yao kwani mafunzo haya yanatukumbusha majukumu  yetu  mbalimbali ambayo sisi kama viongozi tunapaswa tukayasimamie na yatatupa nyenzo muhimu katika utendaji kazi wetu” alisema.

Mafunzo hayo ya siku tatu ni matokeo ya ushirikiano kati ya Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Chuo cha Uhasibu Arusha ambapo moja ya  lengo  la ushirikiano huo ni kutoa mafunzo ya maadili na utawala bora kwa Viongozi wa Umma.

Mafunzo hayo ya maadili yataendelea kufanyika kwa mwezi Aprili – Juni, 2026 ambapo kutakua na mafunzo ya Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Taasisi za Umma na Wakurugenzi wakuu wa Taasisi na Mashirika ya Umma tarehe 22-24 Aprili,2026 Jijini Arusha, Wajumbe wa Bodi za Taasisi na Mashirika ya Umma tarehe 03 -05 Mei,2026 Jijini Mwanza, Wakuu wa Idara na Vitengo katika Wizara, Idara za Serikali Taasisi za Umma, Mamlaka za Serikali na Mashirika ya Umma tarehe 10-12 Juni,2026 Jijini Arusha na 24-26 Juni,2026 Jijini Mwanza.

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >