JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Simbachawene: Tujikite katika kuzuia rushwa badala ya kupambana madhara yake.
05 Dec, 2023
Simbachawene: Tujikite  katika kuzuia rushwa badala ya kupambana madhara yake.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene amezitaka taasisi zinazohusika na kusimamia utawala bora nchini, kujikita Zaidi katika kuzuia vitendo vya rushwa hususani kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo badala ya kusubiria mpaka rushwa itokee ndipo  wanaanza  kupambana nayo.

“Wakati mwingine tunaweka nguvu kubwa na rasilimali nyingi katika kupambana na rushwa wakati ambapo matokeo ya rushwa yanakua tayari yameshatokea na kuleta madhara kwa serikali badala yake tulipaswa kutumia nguvu hiyo hiyo katika kuzuia rushwa isiweze kutokea” alisema.

Mhe. Simbachawene alisema hayo kwenye kongamano la jukwaa la kitaifa la wadau wa juhudi dhidi ya rushwa lililofanyika  tarehe 04 Desemba , 2023 ikiwa ni sehemu ya  maadhimisho ya wiki ya maadili na haki za binadamu  nchini ambapo kilele chake ni tarehe 10 Desemba,2023. Kauli mbiu ya maadhimisho hayo ni “Zingatia Maadili, Utu, Uhuru, na Haki kwa watu wote kwa maendeleo endelevu”

Katika hotuba yake  Mhe. Simbachawene alibainisha  kuwa kutokana na tafiti mbalimbali zilizofanywa nchini ikiwemo tafiti kuhusu hali ya ya Utawala Bora nchini zimebaini kuwa rushwa ni mojawapo ya changamoto katika ufikiwaji wa lengo la serikali la kuhakikisha kuwa wananchi wanapata maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, miundombinu, maji na nk.

“Niwahakikishieni Serikali yetu haitaacha kukabiliana na vitendo vya rushwa na kupambana inapobidi kwa kuwa zipo njia mbalimbali za kuzuia rushwa isiweze kutokea mojawapo ni hii ya kujadili pamoja mbinu za kuboresha zaidi usimamizi wa miradi ya maendeleo” alisema.

Katika hatua nyingine Mhe. Simbachawene alieleza kuwa  matarajio ya Serikali  kupitia mdahalo huo ni kupata mbinu mpya na mawazo mapya ya namna ya kuweza kupambana na rushwa ili kuweza kukuza Maadili nchini .

“Ni Imani yangu kuwa wadau wa sekta zote kwa umoja wetu tutatenda haki kwa mada zitakazowasilisha kwenye jukwaa ili kuweza kutoka na maazimio yatakayosaidia juhudi za kuzuia Rushwa badala ya  kusubiri na kupambana wakati tumeshapoteza rasilimali nyingi” alisema.

Awali akitoa neno la utangulizi Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ambaepia  ni mwenyekiti wa maadhimisho hayo Mhe. Jaji (Mst) Sivangilwa Mwagesi alisema kuwa

moja kati ya shughuli zilizopanga kutekelezwa katika maadhimisho ya mwaka huu ni Jukwaa  la kitaifa la Wadau wa Juhudi ya Rushwa ambalo linakutanisha wadau mbalimbali kutoka Taasisi za Umma watakao jadili kwa kina kuhusu uadilifu wakati wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Mhe. Jaji (Mst) Sivangilwa Mwagesi alieleza kuwa kila tarehe 10 desemba, Tanzania huungana na nchi nyingine Duniani kuadhimisha siku ya Haki za Binadamu Kimataifa ambalo chimbuko lake ni tamko la Haki za Binadamu liililopitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, tarehe 10 Desemba, 1948 (Universal Declaration of Human Rights - UDHR).

Siku ya Maadili na Haki za Binadamu hapa nchini ilianza kuadhimishwa kwa pamoja mwaka 2016 ikiwa ni muunganiko wa siku mbili yaani siku ya Maadili na Haki za Binadamu.

Maadhimisho hayo huratibiwa na taasisi zinazosimamia utawala bora ikiwa ni pamoja na  Ofisi ya Rais Ikulu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Sekretarieti ya Maadili ya  Viongozi wa Umma, Wizara ya Katiba na Sheria, Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa, Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi, Tume ya Utumishi wa Umma, Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi, Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali pamoja na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >