JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Sekretarieti ya Maadili yashiriki kikamilifu Wiki ya Utumishi wa Umma 2025
23 Jun, 2025
Sekretarieti ya Maadili yashiriki kikamilifu Wiki ya Utumishi wa Umma 2025

Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma imeshiriki katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.

Maadhimisho hayo yaliyozinduliwa rasmi Juni 17, 2025 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene (Mb) yamefika tamati Juni 23, 2025 ambapo mgeni rasmi alikua Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (Mb).

Maadhimisho ya mwaka huu, yaliambatana na maonyesho kadha wa kadha kutoka katika Wizara, Taasisi za Umma, Sekretarieti za Mikoa, Asasi za Kiraia na Sekta Binafsi.

Katika maadhimisho hayo, Sekretarieti ya Maadili ilitoa elimu ya Sheria ya Maadili, Mgongano wa Maslahi pamoja na ujazaji wa Tamko la Rasilimali na Madeni kwa njia ya mtandao yaani Online Declaration System (ODS) kwa Viongozi wa Umma na wananchi waliotembelea banda la ofisi hiyo.

Baadhi ya wageni waliotembelea banda la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma walifurahia huduma iliyotolewa na kupongeza jitihada za ofisi hiyo katika kusimamia maadili nchini ikiwemo matumizi ya Mfumo wa ODS unaotumiwa na viongozi kujaza Tamko la Rasilimali na Madeni.

Mmoja wa Viongozi wa Umma aliyetembelea banda la Sekretarieti ya Maadili ni Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile (Mb) ambaye amepongeza jitihada za Sekretarieti ya Maadili kuanzisha mfumo wa ODS ambao kwa mtazamo wake umeleta mabadiliko ya ujazaji wa Tamko la Rasilimali na Madeni kwa Viongozi wa Umma.

“Mnafanya kazi nzuri sana. Licha ya changamoto za kimtandao lakini nilifanikiwa kujaza tamko langu mapema na kwa wakati na kuliwakilisha kwa Kamishna wa Maadili. Rai yangu kwenu ni kuufanyia mfumo maboresho madogo madogo yanayoweza kuathiri ufanisi wake,’’ alisema Mhe. Kihenzile.

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Dkt. Tausi Kida ameunga mkono matumizi ya Mfumo wa ODS na kushauri Sekretarieti kuandaa mafunzo maalum kwa wenza wa Viongozi ili nao wapate uelewa wa masuala ya ujazaji wa Tamko ili iwe rahisi nao kushiriki.

“Wenza wengi wa Viongozi hawafahamu vizuri  jambo hili, hivyo naomba wakati wa kutoa mafunzo kwa Viongozi basi wenza wao wawepo ili waweze kupata uelewa  wa namna suala hilo lilivyo na umuhimu kwa Kiongozi,’’ alisema.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deus Clement Sangu (Mb) ameipongeza Sekretarieti ya Maadili kwa kazi kubwa wanayofanya ya kusimamia maadili kwa Viongozi wa Umma nchini.

“Mnafanya kazi kubwa katika kuhakikisha Viongozi wa Umma wanazingatia maadili wanapotekeleza majukumu yao, nawapongeza  katika hili na pia ninawaomba muendelee na kasi hii katika kuhakikisha tunakua na Viongozi waadilifu nchini,’’ alisema Mhe. Sangu.

Kuhusu Mfumo wa ODS, Naibu Waziri huyo amesema umeleta wepesi kwa vingozi  na ameitaka Sekretarieti ya Maadili kuufanyia maboresho zaidi ili Viongozi waweze kujaza taarifa zao bila changamoto na kwa wakati.

“ODS inafanya vyema tofauti na mwanzo ambapo Viongozi walijaza kwenye makaratasi, kwa njia hii ya mtandao ni rahisi kuwasilisha Tamko kwa wakati, nakumbuka mwaka jana mfumo ulileta changamoto mwishoni na siku za kuwasilisha Tamko zikaongezwa, hivyo naomba mzifanyie kazi changomoto hizo kwa kuboresha baadhi ya maeneo ili mfumo uwe imara zaidi,’’ alisisitiza Mhe. Sangu.

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >