JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Sekretarieti ya Maadili yafungua Klabu za Maadili wilayani Manyoni
30 Apr, 2025
Sekretarieti ya Maadili yafungua Klabu za Maadili wilayani Manyoni

 

Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kupitia Kanda ya Kati, Dodoma, imefungua Klabu mpya 10 pamoja na kuhuisha klabu 06 za Maadili katika wilaya ya Manyoni mkoani Singida ili kuwaandaa na kuwajengea wanafunzi uzalendo na uadilifu kwa Taifa letu.

Zoezi la uanzishaji wa klabu za Maadili lilifanyika kati ya tarehe 22 hadi 25 Aprili, 2025 katika shule za msingi za msingi na sekondari.

Shule za msingi zilizoanzisha klabu mpya za maadili ni Mbwasa, Sukamajela, Sayuni, Solya, Muhalala , Umoja, National, na sekondari ni Solya, Mtori na Mwanzi. Aidha klabu zilizohuishwa ni pamoja na klabu ya shule ya msingi Bomani, Manyoni, Mwembeni, Majengo,Tambukareli na kwa upande wa sekondari ilihuishwa klabu ya shule ya Manyoni.

Akizungumza wakati wa uanzishwaji na uhuishwaji wa klabu hizo Afisa Maadili Sekretarieti ya Maadili Bw. Christian Kapere alisema kuwa Taasisi  imeona ni vyema kuanzisha klabu za maadili katika taasisi za elimu na kuhuisha klabu ambazo zilikua hazifanyi vizuri ili kukuza kizazi na jamii adilifu.

“Tumekuja kuanzisha klabu za Maadili katika shule hizi tukiamini kwamba Viongozi watakaoongoza Taifa hili hapo baadaye wapo miongozi mwenu. Hivyo, ni dhahiri kuwa mnapaswa kupewa elimu ya maadili ili kuwandaa kuwa viongozi waadilifu na wazalendo mtakaofanya maamuzi kwa manufaa ya jamii nzima,” alisema.

Bw, Kapere alieleza kuwa klabu za Maadili katika ngazi za shule za msingi, sekondari na vyuo zina umuhimu mkubwa kwani elimu inayotolewa, itasaidia kuwajengea wanafunzi misingi bora ya maadili mapema na kuzuia vitendo vya mmomonyoko wa maadili

Miongoni mwa mambo muhimu yanayofundishwa katika klabu za Maadili ni uwajibikaji, uzalendo, heshima, kujali watu wengine, kusema ukweli na kuwa mzalendo kwa nchi yako.

“Sote tunafahamu kuwa malezi yanachangia kwa asilimia kubwa kuamua hatma ya watoto wetu hapo baadae, ndio maana waswahili wanasema, samaki mkunje angali mbichi, basi nasi tumekuja kuanzisha klabu hizi ili tuweze kutoa elimu hii ya maadili tukiamini kuwa watoto hawa watakua na kuishi nayo mpaka watakapokua wakubwa,” alisema.

Katika hatua nyingine Mwalimu Mkuu wa Shule ya msingi Mbwasi wilayani Manyoni ambae pia ni mlezi wa klabu ya Maadili shuleni hapo Mwl. Anna Minja  alisema kuwa klabu hizo zitakua na manufaa makubwa shuleni hapo kwani zitasaidia wanafunzi kuishi kwa kuzingaia misingi bora ya uadilifu na kuongeza ufaulu katika masomo yao.

“Kwa upande wetu, tumefarijika sana na uanzishwaji wa klabu za Maadili kwani zitatusaidia kujengea wanafunzi wetu misingi bora itakayosaidia kuongeza uadilifu na kukuza ufaulu kwa wanafunzi wetu.”

“Sisi tutajitahidi kutoa elimu ili kuhakikisha klabu hizi zinafanikiwa na kuleta mabadiliko katika jamii yetu,” alisema.

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >