JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

MWANGESI: VIONGOZI JITOKEZENI KWENYE MAFUNZO YA MAADILI
11 Oct, 2025
MWANGESI: VIONGOZI JITOKEZENI KWENYE MAFUNZO YA MAADILI

 

Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi ametoa wito kwa Viongozi wa Umma nchini kujitokeza kwa wingi kushiriki mafunzo ya maadili awamu ya pili ambayo yataanza mwezi Novemba, 2025.

Wito huo umetolewa jijini Arusha tarehe 10 Oktoba, 2025 kwenye kikao maalum cha kupokea taarifa ya awali ya mafunzo ya Maadili kwa viongozi pamoja na kupokea mpango kazi wa mafunzo kwa awamu ya pili unaotarajia kuanza hivi karibuni.

“Mafunzo haya yatasaidia kupunguza mienendo mibaya kwa kada mbalimbali katika Utumishi wa Umma na pia itawasaidia Viongozi kuwa waadilifu hasa katika kufanya maamuzi kwa kufuata misingi ya sheria, kanuni na taratibu zilizopo katika Utumishi wa Umma,’’ alisema Jaji Mwangesi.

Aidha Jaji (Stahiki) Mwangesi ameziomba timu za wataalamu kutoka Sekretarieti ya Maadili pamoja na Chuo cha Uhasibu Arusha kujipanga vyema katika kutekeleza kikamilifu mpango wa mafunzo hayo kwa awamu ya pili ili kuwafikia Viongozi wengi na kuzidi kuimarisha Utawala Bora.

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) Dkt. Grace Idinga amesema kuwa mafunzo ya awali yalikuwa na ufanisi mkubwa na Viongozi waliyapenda na waliomba kuwepo na mkakati wa kuwafikia Viongozi wengi hasa wa chini kama Wakuu wa Idara na Vitengo.

“Katika awamu ya kwanza kuna makundi ya Viongozi hatukuwafikia hivyo awamu hii tumepanga tuwafikie kwa idadi kubwa hasa wale wa chini kama vile Wakuu wa Idara, Wakuu wa Vitengo, Wenyeviti wa Halmashauri pamoja na kamati zao,” alisema, Dkt. Idinga.

Aidha Dkt. Idinga ameongeza kuwa kama kuna Taasisi ambayo itakua tayari kwa kuwaweka pamoja viongozi wao kwa ajili ya kupata mafunzo hayo, fursa hiyo ipo wazi na wao watakua tayari kufika popote kwa ajili ya kutoa mafunzo hayo.

Mnamo Machi, 2025 Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) walizindua hati ya makubaliano ya kukuza maadili kwa Viongozi wa Umma ambapo awamu ya kwanza ilifanyika Mei na Juni, 2025 na kwa sasa mpango wa mafunzo hayo kwa awamu ya pili unatarajia kuanza Novemba, 2025 ukiwa na lengo kuu la kuboresha utoaji wa huduma kwa jamii nchini.

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >