Sekretarieti ya Maaadili wapigwa msasa namna ya kukuza Maadili kwa njia ya vyombo vya Habari
Viongozi na Maafisa Maadili kutoka Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma wamepatiwa mafunzo ya namna ya kutumia vyombo vya habari katika kukuza maadili kwa Viongozi wa Umma na wananchi kwa ujumla.
Mafunzo hayo maalamu yenye lengo la kuwajengea uwezo maafisa hao katika kuandaa na kuwasilisha mada kwa hadhira kwa kutumia njia za kisasa yanafanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Flomi mjini Morogoro kuanzia tarehe 4 hadi 8 Mei, 2026.
Akifungua mafunzo hayo, Kamishna wa Maadili nchini, Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi amewataka wakufunzi wa mafunzo hayo kuwapitisha washiriki katika mada ambazo zitawasaidia katika kutoa elimu ya maadili kwa umma.
"Mafunzo haya yanakwenda moja kwa moja kwenye kiini cha jukumu letu kuhakikisha ujumbe wa maadili unawafikia walengwa kwa lugha inayofaa kwa hoja zinazojengwa kwa kupitia Sheria, taratibu na kanuni na pia kwa kutumia mbinu zinazoendana na mazingira ya sasa ya mawasiliano" alisema Mhe. Mwangesi.
Jaji Mwangesi ameeleza kuwa baada ya washiriki kupata mafunzo hayo ni matumaini yake kuwa yatawasaidia katika kuboresha maeneo muhimu kama vile kujenga uwezo wa kutambua hadhira, kuandaa maudhui ya maadili yenye mifano halisi, kushiriki kwa kujiamni kwenye vipindi mbalimbali kupitia vyombo vya habari kama, redio, televisheni pamoja na hadhara mbalimbali.
Aidha, Jaji Mwangesi amesisitiza kuwa mafunzo hayo yanatasaidia kuwasiliana kwa ustaha na weledi pamoja na kutumia vizuri mitandao ya kijamii kwa munufaa ya Taasisi katika kutoa elimu, kwani elimu ya maadili sio kusoma vifungu vya sheria tu bali ni uwezo wa kutafsiri Sheria na Sera katika ujumbe unaoeleweka katika mazingira halisi.
Wabobezi wa Tasnia ya habari ambao ni Dkt. Dotto Bulendu kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustne(SAUT)-Mwanza na Dkt. Egbert Mkoko kutoka Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam (UDSM) idara ya Uandishi wa habari na Utangazaji (SJMC).
Baadhi ya mada zinazowasilishwa katika mafunzo hayo ni njia bora ya uwasilishaji wa mada mbalimbali kupitia hadhira tofauti, namna ya kutoa elimu kwa umma na jinsi ya kufanya hamasa pamoja na jinsi ya kujiandaa pindi muhusika anapotaka kwenda kutoa elimu ya maadili kupitia Redio, Televisheni na mitandao ya kijamii.
