KAMATI YA BUNGE IMETOA MIEZI MITATU KUKAMILIKA KWA JENGO LA MAADILI MWANZA.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imetoa miezi mitatu kwa Serikali kukamilisha ujenzi wa jengo la Maadili lililopo wilayani Ilemela mkoani Mwanza likiwa tayari kwa ajili ya kutoa huduma..
Mwenyekiti wa Kamati, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) amemtaka Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kuhakikisha jengo linakamilika ifikapo mwezi Juni, 2026 na kuialika kamati ije kuzindua jengo hilo.
Maagizo hayo yametolewa na Mwenyekiti wa Kamati, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) wakati kamati yake ilipotembelea na kukagua mradi huo tarehe 15, Machi 2026.
“Hapa tumemsikiliza Kamishna wa Maadili akisema jengo linatakiwa kukamilika ifikapo Aprili, 2026 lakini sisi tukiangalia jinsi lilivyo kwa sasa haiwezekani kwa muda huo jengo likawa limekamilka” Mhe. Ndumbaro.
Pia, Mwenyekiti Ndumbaro amemtaka mkandarasi wa ujenzi wa jengo hilo kufanya kazi kwa haraka kwa kuwa kwakuwa hakuna changamoto ya upatikanaji wa fedha.
“Kwa mkandarasi wa kiwango chako hupaswi kusubiri cheti ndio ulipwe, Serikali haijawai kumuzulumu mtu, wewe fanya kazi maliza utalipwa fedha zako, sisi tunachohitaji kazi hii ikamilike” Mhe. Ndumbaro.
Kamishina wa Maadili, Mhe. Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi, amesema kukamilika kwa jengo la utawala la Maadili Kanda ya Ziwa itakwenda kuokoa fedha shilingi milioni 70 ambazo wanatumia kulipa kodi kila mwaka.
“Taasisi yetu ina Kanda nane na kati ya hizo ni kanda tatu tu ndio zinamiliki majengo na zilizobaki zote zimepangisha hali inayofanya Taasisi kutumia fedha shilingi milioni mia tatu kwa ajili ya pango” Mhe. Mwangesi.
Akiongea katika zoezi hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb) amesema uwepo wa jengo Kanda ya Ziwa utasaidia watumishi kufanya vyema kazi ya kusimamia maadili ya Viongozi wa Umma kwa uhuru na ufanisi mkubwa.
