JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Mkuu wa wilaya ya Tanganyika, mkoani Katavi afikishwa mbele ya Baraza la Maadili kwa madai ya ukiukwaji wa maadili.
04 Jun, 2024
Mkuu wa wilaya ya Tanganyika, mkoani Katavi afikishwa mbele ya Baraza la Maadili kwa madai ya ukiukwaji wa maadili.

Mkuu wa wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi Bw. Onesmo Mpuya Buswelu tarehe 4 Juni, 2024 amefikishwa mbele ya Baraza la Maadili kwa tuhuma za ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Bw. Buswelu anatuhumiwa kwa makosa mawili ambayo ni matumizi ya lugha chafu dhidi ya watumishi wa umma na kukamata watu na kuwaweka ndani kinyume cha sheria.

Kikao cha kusikiliza tuhuma dhidi ya kiongozi huyo kimefanyika katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa jijini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Jaji (Mst.) Rose Teemba na mjumbe wa Baraza hilo Bw. Peter Ilomo.

Wakili wa Serikali Bw. Hassan Mayunga emelieleza Baraza kuwa mlalamikiwa wakati akitekeleza majukumu yake ya kikazi amekuwa akitumia lugha chafu na matusi kwa watumishi na watendaji wa serikali wa halmashauri ya wilaya ya Tanganyika kinyume na kifungu cha 6(1)(a) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Bw. Mayunga alisema, “Mhe. Mwenyekiti mlalamikiwa wakati akiteleza majukumu yake ya kikazi amekuwa akiwakamata na kuwaweka mahabusu wananchi, watumishi wa umma  na watendaji wa serikali wa halmashauri ya wilaya ya Tanganyika kinyume na kifungu cha 6(1) (c) cha Sheria iya Maadili ya Viongozi wa Umma.”

“Kushindwa kutimiza wajibu huo wa kisheria ni ukiukwaji wa maadili ya viongozii wa umma kwa mujibu wa kifungu cha 6 (2) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma,” alisema.

Upande wa mlalamikaji uliwaleta mashahidi watatu ambao ni Bw. Leonard Kansimba, Afisa Uchunguzi wa Sekretarieti ya Maadili, Bw. Raymond Bernard, Mkuu wa Shule ya Sekondari Kakoso, wilayani Tanganyika anayedai kutolewa lugha ya matusi na mkuu huyo wa wilaya na Bw. Primo Amadeo Kampamba, fundi ujenzi kutoka Halmashauri ya wilaya ya Tanganyika aliyelieleza Baraza kuwa Mkuu huyo wa Wilaya alimuweka mahabusu bila kufuata taratibu.

Mlalamikiwa ambaye ni mkuu wa wilaya ya Tanganyika ameyakana mashtaka yote mawili na kudai mbele ya Baraza kuwa tuhuma zote anazotuhumiwa nazo ni za kutengeneza kwasababu amekuwa akisimamia vizuri utekelezaji wa miradi ya maendeleo wiyani humo kwa kuhakikisha fedha za miradi zinatumika ipasavyo bila ubadhilifu wa aina yoyote.

“Katika kutenda kwangu kazi kama mkuu wa wilaya ya Tanganyika sijatumia lugha chafu na za matusi kwa watumishi na watendaji wa wilaya.” Alisema na kuongeza kuwa, kazi hizi za ukaguzi wa miradi sijazifanya peke yangu, nilikuwa na viongozi wengine wa Kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya.

“Kwa ukaribu na udhibiti huo, imepelekea wanaodhibitiwa kutofurahi,” aliliambia Baraza huku akitokwa na machozi.

Baada ya kusikiliza pande zote mbili, Mwenyekiti wa Baraza alimueleza mlalamikiwa kuwa, “tumesikiliza pande zote, sasa liachieni Baraza lifanye upekuzi na tathmini kama kutakuwa na chochote mamlaka yako itakujulisha.”

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >