Fuateni Suluhu ya Vihatarishi kuepuka Madhara kwenye Taasisi.

Kamishna wa Maadili, Mhe. Jaji (Stahiki) Sivangilwa Mwangesi amewataka watumishi kutafuta Suluhu ya vihatarishi vilivyopo katika Taasisi kuepuka madhara yanayoweza kuathiri taswira yake mbela jamii na Viongozi wa Umma.
Mhe. Mwangesi ametoa agizo hilo wakati akifungua kikao kazi cha kuhuisha daftari la viatarishi la Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kilichowakutanisha wawakilishi kutoka kila Idara, Vitengo na Ofisi za Kanda mkoani Morogoro tarehe 30 Aprili, 2025.
Alisema, wakati mnafanyia kazi ya uhuishaji wa daftari, tunategemea utaisaidia Taasisi kuongeza tija katika utekelezaji wa majukumu ya kisheria. Kikao kazi hiki kinapitia daftari la Viatarishi kutambua changamoto zinazokabili Taasisi katika utekelezaji wa majukumu na namna ya kupunguza uwezekano wa kutokea kwake.
“Ni imani yangu kuwa kazi hii ikifanyika vizuri tutafikia matarajio ya wananchi ya kuona viongozi waliopewa dhamana wanatekeleza majukumu yao kwa uadilifu ambalo ndilo lengo kuu la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Taifa kwa ujumla,” amesema.
Kwa mujibu wa Kamishna wa Maadili, uhuishaji wa Dafrati la Vihatarishi, utasaidia Taasisi kuongeza tija kwa kutambua changamoto zinazoikabili na kuzitafutiai ufumbuzi.
“Zoezi hili liongeze tija ndani ya Taasisi, utendaji wetu wa kazi uendane na thamani ya fedha tunayotumia katika utekelezaji wa majukumu yetu,” alisema.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mipango, Ufuatiliaji na Tathmini, Bw. Omary Juma amesema zoezi la uhuishaji wa daftari la Viatarishi utapunguza viatarishi vilivyopo ndani ya Taasisi na kuwa na kuongeza thamani ya fedha.
“Kazi hii inafanyika kwa kuangalia taswira ya Taasisi kwa ujumla na kutafuta ufumbuzi,” alisema.
Naye Mwezeshaji wa mafunzo hayo Bw. Onesmo Mbekenga kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali ametoa wito kwa Taasisi kuwa na mpango thabiti wa kupunguza viatarishi kwa kuweka katika mpango kazi wake wa kila mwaka.