JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

DIWANI WA KATA YA CHEYO AFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI
07 Jun, 2024
DIWANI WA KATA YA CHEYO AFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI

 
 

Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma imemfikisha  Bw. Yusuph Khamis Kitumbo Diwani wa Kata ya  Cheyo Halmashauri ya  Manispaa ya  Tabora mbele ya Baraza la Maadili kwa tuhuma za kushindwa kuwasilisha Tamko la Raslimali na Madeni kwa muda wa miaka minne  mfulululizo.

Kikao  hicho cha Baraza la Maadili kilifanyika  tarehe 7 Juni, 2024 jijini Dodoma katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na kuongozwa na Mwenyekiti wake  Jaji (Mst.) Rose Teemba pamoja na mjumbe wa Baraza hilo Bw.  Peter Ilomo.

Wakili wa Serikali Bw. Hassan Mayunga ameliambia Baraza kuwa, “kitendo cha kiongozi huyo kushindwa kutoa Tamko la Raslimali na Madeni ni ukiukwaji wa kifungu cha 9(1)(b) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.”          

Akitoa ushahidi mbele ya Baraza hilo kwa upande wa mlalamikaji Afisa Uchunguzi  mwandamizi Bi. Halima Ramadhani Mnenge amesema hata baada ya kiongozi huyo kukumbushwa kwa njia ya barua kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya kumtaka atimize wajibu wa kisheria wa kuwasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni, alishindwa kufanya hivyo.

Aidha, shahidi alieleza kuwa pamoja na kiongozi huyo kushindwa kuwasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni kwa muda wa miaka minne mfululizio tangu mwaka 2020, hata alipowasilisha Tamko lake, hakuzingatia muda uliowekwa kwa mujibu wa sheria.

“Mwaka 2015 alipochaguliwa kuwa Diwani wa kata ya Cheyo katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, hakutoa Tamko ndani ya siku 30 kama Sheria ya Maadili inavyomtaka, badala yake alitoa tamko hilo mwaka 2016 baada ya kukumbushwa kwa barua. Mwaka 2017 pia hakutoa Tamko la Rasilimali na madeni kwa wakati,” aliliambia Baraza la Maadili.

Tangu mwaka 2020 hadi 2023, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma haikupokea tamko lake la Rasilimali na Madeni.

Aidha, Diwani huyo katika utetezi wake aliliambia Baraza kuwa yeye hakuwa na Elimu yoyote kuhusu Ujazaji wa Matamko na hajawahi kupata mafunzo yoyote kuhusu Maadili ya Viongozi wa Umma.

“Tangu nilipochaguliwa kuwa diwani wa Kata ya Cheyo mwaka 2015, sijawahi kuhudhuria darasa lolote la masuala ya maadili.’

Hata hivyo amekiri kuchelewesha uwasilishaji wa Tamko la Rasillimali na Madeni la mwaka 2015 na mwaka 2016.

Alisema, “Tamko la mwaka 2015 na mwaka 2016 niliwasilisha kwa kuchelewa wakati matamko ya mwaka 2020 na 2021 niliyawasilisha kwa njia ya barua pepe.”

Baada ya kusikiliza pande zote mbili, Mwenyekiti wa Baraza alimueleza mlalamikiwa kuwa, “tunashukuru, tumesikia utetezi wako Baraza litafanye uchunguzi na kutoa mapendekezo.”

 

 

 

 

 

 

 

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >