JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS – SEKRETARIETI YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

DC ULANGA AFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI KWA TUHUMA ZA MATUMIZI MABAYA YA MADARAKA
27 Oct, 2023
DC ULANGA AFIKISHWA MBELE YA BARAZA LA MAADILI KWA TUHUMA ZA MATUMIZI MABAYA YA MADARAKA

Mkuu wa Wilaya ya Ulanga Mkoani Morogoro, Mhe. Dkt. Julius Kenneth Ningu (59) amefikishwa mbele ya Baraza la Maadili kwa tuhuma za ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ikiwemo matumizi mabaya ya madaraka na lugha za vitisho dhidi ya watumishi wa umma alipokuwa katika ziara za ukaguzi wa miradi mbalimbali.

Akiwasilisha malalamiko hayo mbele ya Baraza Wakili Mkuu wa Serikali Bi. Emma Gelani, ameliambia Baraza la Maadili kuwa Dkt. Ningu alifanya vitendo hivyo kinyume na kifungu cha 6 (1)(a) na 6(1)(b)(i) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma akiwa Mkuu wa wilaya ya Namtumbo, mkoani Ruvuma kabla ya kuhamishiwa wilaya ya Ulanga Mkoani Morogoro.

“Dkt. Ningu wakati akitekeleza majukumu yake amekuwa akiwakamata na kuwaweka mahabusu watumishi wa umma na wananchi kinyume na kifungu cha 6(1)(c) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.”

Kwa mujibu wa Wakili huyo, kushindwa kutimiza wajibu huo wa kisheria ni ukiukwaji wa maadili ya viongozi wa umma kwa mujibu wa kifungu cha 6(2) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Wakili Gelani alisema, “Mhe. Mwenyekiti, kitendo hiki ni kinyume na maelekezo ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupitia barua yake ya tarehe 1/4/2019 kwenda kwa wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kuhusu matumizi sahihi ya Sheria ya Tawala za Mikoa Sura ya 97 inayotoa utaratibu wa kumuweka mtu mahabusu kwa muda wa saa 48.”

Kwa mujibu wa Wakili huyo Mkuu wa Serikali, maelekezo ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, yanamtaka Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa wilaya kutoa maelezo kwa njia ya maandishi kwa jeshi la polisi kabla au muda mfupi baada ya kuamulu mtu kuwekwa ndani kutoa sababu za msingi za kumuweka mahabusu mtuhumiwa.

“Dkt. Ningu hakutoa maelezo yoyote kwa jeshi la polisi kuhusiana na kukamatwa kwa watumishi wa halmashauri na mafundi waliokuwa wakitekeleza mradi ya UVIKO 19 katika wilaya ya Namtumbo kinyume na maelekezo ya Sheria,” alieleza.

Katika shauri hilo Na.1 la mwaka 2023, upande wa Mlalamikaji ulileta mashahidi watatu.

Bw. Mario Fabian Mwageni, Afisa Mtendaji kata ya Rwinga, wilaya ya Namtumbo, Mkoani Ruvuma aliyekuwa shahidi upande wa mlalamikaji, ameliambia Baraza kuwa mnamo tarehe 22/11/2021 Mkuu wa wilaya alipotembelea Kata yake kukagua shughuli za maendeleo alisema, “wewe na mkuu wa shule ya Rwinga lazima niwaweke ndani ili nionyeshe mfano kwa watumishi wengine kwasababu mnakwamisha shughuli za ujenzi wa madarasa.”

Kwa mujibu wa Mtendaji huyo wa Kata, Mkuu wa wilaya “aliamuru tuingie kwenye gari hadi Namtumbo. Tulipofika Namtumbo, alisema DAS (Katibu Tawala wa Wilaya) peleka watu hawa ndani mpaka nitakapoeleza vinginevyo.”

“Tuliwekwa mahabusu tangu saa 7:00 mchana hadi saa 3:00 usiku na tukatolewa bila kuambiwa kosa letu na hakuna chochote kilichoendelea,” alieleza.

Kwa upande wake OCD wa wilaya ya Namtumbo Bw. William Abel Mwamafupa amekili mbele ya Baraza kuwaweka mahabusu watuhumiwa kwa amri ya Mkuu wa wilaya bila maelezo.

“Mkuu wa wilaya anatakiwa kuniandikia barua anapotoa amri ya kuwaweka watu mahabusu, lakini tulipokuwa tukienda kukagua miradi ya maendeleo Mkuu wa wilaya alikuwa anaamuru wahusika wa miradi iliyokuwa inasuasua wakamatwe na kuwekwa ndani bila maelezo.”

Alipopewa nafasi ya kujitetea, Dkt. Ningu alikana mashitaka hayo na kusema alifanya hivyo kwa kushauriwa na Kamati ya Usalama ya Wilaya.

Utetezi wa pande zote mbili umekamilika.

Mwenyekiti wa Baraza Mhe. Teemba amesema, “Baraza litakaa litafanya kinachopaswa kufanyika kwa mujibu wa sheria.”

Baraza hilo linafanya kikao chake cha siku mbili jijini Dodoma kuanzia tarehe 5 Septemba, 2023 chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Jaji (Mst.) Rose Teemba akisaidiana na Wajumbe wa Baraza Bw. Peter Ilomo na Bi. Suzan Mlawi.

Online Help
Kuanzisha Enzi Mpya katika Udhibiti wa Sekta ya Michezo ya Kubahatisha nchini Tanzania
Ofisi ya maadili inafanya kazi na imewashughulikia viongozi wengi sana kupitia Baraza la Maadili ambalo pia liliendeshwa mwaka 2013 Novemba mkoani Tabora. Viongozi mbalimbali waliokuwa na tuhuma za ukiukaji wa maadili waliitwa kwenye Baraza na kuhojiwa na Baraza linatoa mapendekezo na kuyawasilisha mapendekezo hayo kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi za kinidhamu na kisheria kwa viongozi husika.

" >
Kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Maadili kimeainisha wazi mali zinazotakiwa kutajwa kuwa ni fedha taslimu, fedha zilizopo katika taasisi za kifedha kama vile benki, hisa, nyumba, mashamba, magari, mitambo na mali nyinginezo. Kiongozi anatakiwa kutoa tamko la mali anazomiliki yeye mwenyewe, mke/mume na watoto walio chini ya umri wa miaka kumi na nane. Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni zinatakiwa kujazwa kila mwaka na kiongozi hutumiwa fomu hizo na Ofisi ya Maadili na pia zinapatikana katika mtandao wa maadili yaani www.ethicssecretariat.go.tz. Sheria inamtaka kiongozi kutolea tamko madeni yake ili kuweza kujua kuwa kiongozi anamiliki mali zipi na pia kutambua kuwa amezipata vipi mali hizo ukilinganisha na kipato cha kiongozi husika. Kiongozi kuwa na mali nyingi si dhambi kwani hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetamka wazi kuwa kila raia ana haki ya kumiliki mali ila ofisi inataka kujiridhisha uhalali wa jinsi mali ilivyopatikana. Mapendekezo katika Katiba mpya yanasisitiza maadili kwa kutenganisha uongozi na biashara.

" >
Wananchi wengi wamejijengea dhana kuwa bila pesa huwezi kupata huduma ya kiserikali kitu ambacho si kweli kwani huduma nyingi za kiserikali zinatolewa bure kabisa ila cha msingi wananchi wanatakiwa kutoa taarifa katika vyombo husika pindi wanapotakiwa kulipia huduma ambazo zinatolewa bure. Jamii inatakiwa kubadilika na kuamini kuwa si lazima kutoa rushwa ndipo upate huduma. Wapo wananchi wengi ambao walileta malalamiko kama hayo na Ofisi ya Maadili iliyashughulikia, hivyo wananchi wasisite kutembelea Ofisi zetu kwa ajili ya kutoa taarifa kama hizo.

" >
Kutoa lugha chafu ni ukiukwaji wa maadili. Ndani ya Bunge kuna Kamati ya Maadili ambayo ipo kwa ajili ya kuwawajibisha wabunge wanaotoa lugha chafu. Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa upande wake ilifanya semina kwa wabunge ili kuwakumbusha mipaka ya utendaji kazi na maadili kwa ujumla, na tangu wakati huo matumizi ya lugha chafu bungeni yamepungua kwa kiasi kikubwa.

" >